Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mikakati ya Mwambusi Yanga

98300a6fae45b0b52f29ccb42a2dc669 Mikakati ya Mwambusi Yanga

Sat, 13 Mar 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

KAIMU Kocha Mkuu wa Yanga, Juma Mwambusi amesema wanahitaji kuweka mikakati kulingana na mashindano yaliyoko mbele yao namna gani wajipange kuhakikisha wanatimiza malengo yaliyokusudiwa.

Mwambusi aliyeondoka Yanga Januari mwaka huu kwa madai kuwa anaumwa, amerejeshwa kuitumikia timu hiyo baada ya uongozi wa klabu hiyo kuvunja benchi la ufundi lililokuwa linaongozwa na Cedric Kaze kufuatia kutoridhishwa na mwenendo mbaya wa matokeo.

Akizungumza na gazeti hili Dar es Salaam jana, Mwambusi alisema kitu cha kwanza alichopanga kufanya ni kukutana na wachezaji wote Jumatatu na kufanya nao mazungumzo ili kuweka mikakati sawa.

“Natarajia kukutana na wachezaji na kufanya nao kikao tuweke mikakati yetu kuelekea kwenye mechi za Ligi Kuu, Kombe la FA namna ya kujipanga kufanya vizuri,”alisema.

Kocha huyo wa zamani wa Mbeya City alisema atakuwa na mikakati yake atakayochanganya na ile ya uongozi ambao nao utahitajika kuwasikiliza ili kufanya vizuri zaidi.

Mwambusi alisema tayari amemalizana na klabu hiyo kwa maslahi yake kuendelea kutumikia ajira yake vizuri ipasavyo.

Moja ya malengo waliyonayo Yanga ni kunyakua ubingwa, lakini hivi karibuni ndoto zao zilianza kuyeyuka kutokana na mwenendo mbaya katika baadhi ya mechi za mzunguko wa pili wakionekana kupata sare nyingi kuliko ushindi.

Hata hivyo, Yanga bado iko katika nafasi nzuri ya uongozi ikiwa imecheza michezo 23 na kushinda 14, sare nane na kupoteza mmoja wakiwa na pointi 50.

Matokeo yao ya mechi kadhaa zilizopita yaliwafanya mashabiki kukata tamaa kwenye mbio za ubingwa na kumhofia mtani wake wa jadi Simba huenda akaja kuwashusha kwani yupo nafasi ya pili kwa pointi 46 katika michezo 20 na akicheza viporo vitatu na kushinda anaweza kuwang’oa katika uongozi.

Chanzo: www.habarileo.co.tz