Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mgunda atoboa siri Simba

Mgunda Pic Siri Juma Mgunda

Tue, 1 Nov 2022 Chanzo: Mwanaspoti

Simba imeendelea kunoga baada ya juzi kuichapa Mtibwa Sugar mabao 5-0 kwenye mchezo ya Ligi Kuu uliofanyika Uwanja wa Mkapa, huku kocha Juma Mgunda akisifia kiwango cha nyota wake, hasa washambuliaji.

Mgunda alisema haikutokea ghafla kushinda mabao matano ambayo ni mengi kufungwa kwenye mchezo mmoja na timu moja kwenye ligi msimu huu, lakini ni maandalizi makubwa waliyofanya mazoezini.

Alitaja eneo la ushambuliaji lililo chini ya Moses Phiri, Agustine Okrah, Pape Sakho Habib Kyombo na Clatous Chama kumkosha zaidi kwa kile wanachokifanya na kuwataka kuendelea kufanya vizuri zaidi katika mechi zijazo.

Hadi sasa, Simba ndiyo inaongoza kwa mabao mengi kwenye ligi (17) na kuwa timu iliyofungwa machache zaidi (4), huku Safu yake ya ushambuliaji ikiwa ndiyo inaongoza kwa kupachika mabao mengi.

Mabao hayo 17 ya Simba, 14 yamefungwa na washambuliaji akiongoza Phiri mwenye matano, akifuatiwa na Okrah (matatu), Sakho na Kyombo (mawili), Chama (moja) na Dejan Georgijevic aliyeondoka na bao moja, huku mengine mawili yakifungwa na viungo Mzamiru Yassin na Jonas Mkude wenye na lingine likiwa la kujifunga kwa beki wa Dodoma Jiji, Abdallah Shaibu ‘Ninja’.

Mgunda alisema makali hayo ya kikosi chake, yanakuja kutokana na namna anavyokaa na nyota wake na kuwafundisha namna ya kucheza kama timu ili kufunga zaidi na kuipa timu matokeo chanya.

“Kadri siku zinavyozidi kwenda naona mabadiliko mazuri ndani ya kikosi changu na wachezaji wanaanza kucheza vile ninavyotaka na tunavyowaelekeza mazoezini,” alisema kocha huyo wa zamani wa Coastal Union.

Mgunda aliichukua Simba Septemba 8, akiwa kama kaimu kocha akitokea Coastal Union na kuziba nafasi iliyoachwa na Mserbia Zoran Minojlovic na tangu ameichukua ameiongoza kwenye mechi tano za ligi akishinda tatu, sare moja na kupoteza moja, huku akishinda nne za Ligi ya Mabingwa.

Chanzo: Mwanaspoti