Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mfungaji Bora Norway aitwa Taifa Stars

Amahl Pellegrino (15).jpeg Mfungaji Bora Norway aitwa Taifa Stars

Wed, 20 Dec 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Mfungaji bora wa Ligi Kuu Norway 'Eliteserien', Amahl Pellegrino ambaye anaichezea Bodo/Glimt ya nchini humo ni miongoni mwa wachezaji 53 ambao wameitwa na Adel Amrouche kwenye kikosi cha awali cha Taifa Stars kwa ajili ya maandalizi ya fainali za mataifa ya Afrika (Afcon).

Tanzania ni miongoni mwa mataifa 24 ambayo yatapigania ufalme wa Afrika huko Ivory Coast ambako fainali hizo zitafanyika Januari 13 hadi Februari 11 mwakani kwa mara ya 34 huku ikiwa mara ya pili kwa taifa hilo kuwa mwenyeji, mara yao ya kwanza ikiwa 1984.

Pellegrino ambaye amezaliwa na kukulia Norway ni ingizo lingine jipya kwenye kikosi hicho ambacho kwa miaka ya hivi karibuni kimekuwa kikitoa nafasi kwa wachezaji wenye asili ya Tanzania wanaofanya vizuri kwenye mataifa mbalimbali yaliyoendeleza zaidi kisoka.

Mshambuliaji huyo mwenye miaka 33, alikuwa akipigiwa debe na wadau mbalimbali wa soka la Tanzania kutokana na kufanya kwake makubwa kuanzia kwenye ligi za ndani Norway hadi upande wa michuano ya Ulaya ambayo Bodo/Glimt imekuwa ikishiriki na kufanya vizuri.

Akiwa na Bodo/Glimt, msimu uliopita nyota huyo mwenye asili ya Zanzibar alikuwa mfungaji bora wa Eliteserien baada ya kumaliza msimu akiwa na mabao 24 yaliyoisaidia timu yake kuchukua ubingwa wa ligi. Pia ni kati ya wachezaji muhimu walioifanya Bodo/Glimt kutinga mtoano wa Europa Conference League baada ya kufanya vizuri katika hatua ya makundi.

Mbali na Pellegrino majina mengine mapya kwenye kikosi hicho cha awali ni pamoja na wadogo zake na mchezaji wa zamani wa Chelsea, Adam Nditi ambao ni Zion (Aldershot Town) na Roberto (Forfar Athletic).

Wengine ni Ayoub Bilal (FK Gorazde), Tarryn Allarakhia (Wealdstone), Miano Danilo na Twariq Ahmed (Telford United), Mark John (Kingstone), Mohammed Ali (Boreham Wood), Adam Kasa (IFK Haninge), Said Khamis (FK Jedinstvo), Cyprian Kachwele wa Vancouver Whitecaps FC 2.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live