Goat, Lionel Messi amelitaja bao lake analolipenda kati ya mabao yanayokaribia 850 aliyofunga kwenye maisha yake ya soka.
Gwiji huyo wa Argentina, Messi, anatajwa mmoja kati ya wanasoka bora wa muda wote. Na rekodi yake ya kufunga imekuwa haina mjadala tangu alipoanza kukipiga akiwa mdogo kwenye kikosi cha Barcelona. Lakini, Messi ametaja bao lake alilopenda zaidi kati ya mabao 848 aliyofunga kwenye maisha yake ya soka.
Na bao hilo ni lile juhudi binafsi aliloifunga Real Madrid katika nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya mwaka 2011. “Bao ambalo siku zote nitalikumbuka, ni lile nililofunga dhidi Madrid, tuliipiga 2-0 kwenye nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya uwanjani Bernabeu,” alisema Messi.
Messi alichukua mpira katikati, akagongeana pasi na Sergio Busquets akawazunguka viungo Xabi Alonso na Lassana Diara. Akawalamba chenga Raul Albiol, Sergio Ramos na Marcelo kabla ya kufunga kwa mguu wa kushoto.