Licha ya KMC kulazimishwa sare ya bao 1-1 na Tanzania Prisons katika mchezo wa Ligi Kuu Bara uliopigwa kwenye Uwanja wa Uhuru, ila kocha mkuu wa timu hiyo, Abdihamid Moallin amesema anafurahishwa na maendelezo ya kikosi hicho hadi sasa.
Mchezo huo uliochezwa juzi uliifanya KMC kufikisha michezo mitano mfululizo bila ya kupoteza tangu mara ya mwisho timu hiyo ilipofungwa kipigo cha fedheha cha mabao 5-0, dhidi ya Yanga Agosti 23, mwaka huu kwenye Uwanja wa Azam Complex.
Akizungumza na Mwanaspoti jijini Dar es Salaam, Moallin alisema malengo yao yalikuwa ni kupata pointi tatu katika uwanja wa nyumbani lakini kutokana na ubora wa wapinzani wao hasa kwenye kuzuia uliwanyima nafasi hiyo ya kutimiza walichotaka.
"Tulicheza na timu nzuri ambayo ina uwezo mkubwa wa kuzuia, sare sio mbaya sana kwa sababu hatujapoteza ila tunahitaji zaidi kuboresha kila eneo ili kuendeleza ubora wetu, kwani malengo yetu bado ni kushikilia nafasi nne za juu," alisema.
Moallin aliyeshinda tuzo ya kocha bora Septemba aliongeza siri kubwa ya mwendelezo mzuri ni wimbi kubwa la vijana wenye vipaji.
"Tuna wachezaji wengi vijana wenye kiu na shauku kubwa ya kufikia mafanikio, hii kwetu inatusaidia kwa sababu unaona tu jinsi wanavyocheza na wanavyoipigania timu katika kila mchezo jambo ambalo linaleta athari chanya ya moja kwa moja."
KMC inaendelea kusalia nafasi ya nne na pointi 12 katika michezo saba iliyocheza ambapo imeshinda mitatu, sare mitatu na kupoteza mmoja.