Mabao ya haraka yaliyofungwa na straika Chrispin Ngushi yameiwezesha Mbeya Kwanza kuondoka na pointi moja dhidi ya Mbeya City katika mchezo wa Ligi Kuu uliopigwa leo Jumapili, Oktoba 3.
Mechi hiyo ambayo ilikuwa kali kwa timu zote, Mbeya City ndio walitangulia kupata mabao yao kupitia kwa Paul Nonga dakika ya 45 kisha Richardson Ng'ondya dakika ya 79.
Mbeya Kwanza walicharuka dakika za mwisho na kutengeneza mashambulizi kadhaa na kufanikiwa kupata bao la kwanza dakika ya 80 kupitia kwa Ngushi kisha kupigilia la pili dakika ya 88 akifunga kwa 'tiktaka' na kujikuta akiumia wakati akishangilia kwa kuruka sarakasi.
Hata hivyo Mbeya City walikosa penalti katika dakika za mapema kupitia kwa Eliud Ambokile ambaye mkwaju wake ulipanguliwa na Kipa, Hamad Juma.
Akizungumza baada ya mchezo huo, Kocha Mkuu wa Mbeya Kwanza, Harerimana Haruna amesema walipoteza umakini dakika za awali na kuwatuliza vijana wake na kuwataka kupambana na kuweza kupata sare hiyo dakika za mwisho.
"Hatukuwa na utulivu mapema lakini baadaye niliwatuliza na kuanza kucheza kwa utulivu, nashukuru kwa pointi hiyo moja japokuwa tulihitaji alama tatu" amesema Haruna.
Kwa upande wake Kocha wa Mbeya City, Mathias Lule amesema umakini kwa vijana wake dakika za mwisho ndio kulisababisha wanakosa alama tatu ambazo walikuwa wameshaziandika.
"Umakini ulipungua dakika za mwisho na kuwafanya wapinzani kuweza kupata sare hii, tutarekebisha katika mechi zinazofuata" amesema Lule.