Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mazembe vs Esperance ni bonge la mechi kwa Mkapa

Mazembe Vs Esperence Mazembe vs Esperance ni bonge la mechi kwa Mkapa

Sun, 22 Oct 2023 Chanzo: Mwanaspoti

Leo ndani ya Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam kinawaka tena, wakati ambapo TP Mazembe watakuwa uwanjani kuvaana na Esperance ya Tunisia kwenye michuano mipya ya African Football League.

Mchezo huo awali ulitarajiwa kupigwa nchini DR Congo, lakini baadaye ulihamishiwa kwa Mkapa na baada ya mashabiki kumaliza kutazama mechi kali ya juzi kati ya Simba na Ahly, hii ni nyingine baab’kubwa.

Mazembe kwa Afrika ni timu tishio ikiwa imetwaa Ligi ya Mabingwa mara tano nyuma ya Al Ahly iliyofanya hivyo mara 11. Pia imebeba Kombe la Shirikisho Afrika mara mbili mfululizo a 2016 na 2017. Katika miaka ya karibuni, Mazembe walionekana kulala, lakini msimu huu wameamka na kufanya usajili mzuri wakiwa wanaongoza kwenye Ligi Kuu DR Congo.

Hii ni miongoni mwa timu zenye heshima kubwa kwenye soka la Afrika ikiwa imeshazalisha mastaa wengi wakubwa.

Mazembe tayari imetinga makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwa msimu huu kitu ambacho ilishindwa kufanya msimu uliopita baada ya kuifunga Nyassa Big Bullets ya Malawi. Jopo lake lote chini ya tajiri Moise Katumbi lipo Dar es Salaam, na juzi alikuwa shuhuda wakati Simba wakipasuana na Ahly.

Ukubwa wa Esperance ambao wametwaa Ligi ya Mabingwa Afrika mara nne, ndiyo unachangia mechi hii kuwa kubwa. Hadi sasa inaongoza ligi ya Tunisia ikiwa imecheza mechi tano, kushinda nne na sare moja ikivuna alama 13.

Ipo tayari kwenye makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika ikiitoa Douanes. Mazembe na Esperance zimekutana mara saba katika michuano tofauti na wakati tofauti ambapo Esperance inaonekana kuwa na rekodi tamu zaidi kwani imeshinda mara tatu na kutoa sare mara mbili huku Mazembe ikishinda mara mbili tu.

Hii ni mechi nyingine kali ambayo mashabiki wanatakiwa kwenda kuitazama kwa Mkapa.

Pale Nigeria kinawaka pia wakati Enyimba watakapovaana na Wydad Casablanca ya Morocco.

Timu hizo zimekutana mara moja tu na ubora wao unatenganishwa na daraja, Enyimba ikiwa timu pekee inayocheza leo ambayo imeshatupwa nje kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika.

Chanzo: Mwanaspoti