Zikiwa zimebaki siku 3 kuingia mwaka 2023, kuna matukio mbalimbali yaliyotokea kwenye soka ambayo yaliishangaza jamii na kujadiliwa kwa muda mrefu kwenye mitandao ya kijamii na vijewe mbalimbali.
TUISILA KISINDA - YANGA
Usajili wa winga wa Yanga, Tuisila Kisinda kurejea Yanga akitokea RS Berkane ya Morocco kupitia usajili wa dirisha kubwa, ulizua gumzo, huku mashabiki wa Yanga wakichelea kuongezwa nguvu kwenye kikosi chao, watani wao wa jadi wakiponda kafulia.
Kwa mara ya kwanza kucheza Yanga ilikuwa 2020/21, baada ya kuonyesha kiwango cha juu akapata ofa ya Morocco na mbadala wake akawa Jesus Moloko lakini akarejea tena kwa mkopo.
HABIBU KYOMBO - SIMBA
Kilichofanya usajili wa straika wa Simba, Habibu Kyombo akitokea Mbeya Kwanza ujadiliwe zaidi kwanza mashabiki hawakutarajia kupata ugeni huo.
Kitendo cha Simba kuwatema mastraika wake Meddie Kagere na Chris Mugalu walitegemea wangeshushiwa staa mwenye rekodi ya mabao, ingawa Kyombo alimaliza na mabao saba Mbeya Kwanza, jambo lingine ni alidabo saini alitangulia kutangazwa kuwa amemwaga wino Singida Big Stars lakini baadaye akaibukia Simba.
STEPHAN AZIZ KI - YANGA
Kiungo mshambuliaji wa Yanga, Aziz Ki aliyesajiliwa kutoka Asec Mimosas ya Ivory Coast alitambulishwa usiku wa manane na usajili wake ulichukua muda wa wadau wa soka kumjadili kwa ubora wake aliokuwa ameuonyesha kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika, pia kitendo cha Simba kuikosa saini yake kiliendeleza gumzo zaidi.
BERNARD MORRISON - YANGA
Zilianza tetesi kabla ya kumaliza mkataba wake Simba 2021/22, winga huyo anarejea Yanga ambako ilikuwa timu yake ya kwanza kuichezea hapa nchini mwaka 2020 alicheza miezi sita tu, hivyo usajili wake ulizua mjadala mkubwa mbele ya mashabiki kwa kuwa pia alishawahi kuitumia Yanga.
ALI AHMADA - AZAM FC
Ulikuwa ni kati ya sajili kubwa zilizofanywa na Azam FC, kumchukua kipa Ali Ahamada (30) kutoka Sportskubben ya Norway aliyekuwa na uzoefu mkubwa na michuano ya kimataifa, alianza vizuri Ligi Kuu na michuano ya CAF, ingawa kwa sasa anaonekana ameruhusu mabao mengi.
ABDUL SELEMAN ‘SOPU’-AZAM
Kutokana na kiwango alichokionyesha wakati akiwa na Coastal Union ya Yanga, ndiyo ikawa sababu ya Azam kuzishinda Simba na Yanga kwa kufanikisha saini yake, ulikuwa ni kati ya sajili zilizojadiliwa, aliwafunga Yanga kwenye fainali ya Kombe ASFC baada ya kufunga mabao matatu hat trick, tetesi zikasema anakwenda Simba au Yanga lakini ghafla akaibukia Azam .
TIGERE, WADADA- IHEFU
Kitendo cha Ihefu kusajili majina makubwa, kiungo Never Tigere na beki Nicholas Wadada wote ni wakigeni, ulifanya usajili wao kujadiliwa na kuona timu hiyo ingeanza na ushindani mkali ingawa mambo yaliwaendea kombo.
Beki wa zamani wa Simba, Mohamed Banka anasema mastaa hao wanapaswa kujitathimini kama wamekifanya kile kilichokuwa kinatarajiwa na mashabiki wao.