Mchezaji wa zamani wa Simba na Timu ya Taifa ya Tanzania, Jamhuri Kihwelu 'Julio' ameonesha kuhuzunishwa na matokeo mabovu ya Taifa Stars kwenye michuano ya AFCON inayoendelea nchini Ivory Coast.
Julio amesema hayo mara baada ya Stars kushindwa kulinda bao walilofunga dakika za awali na kusababisha kutoa sare dhidi ya Zambia.
“Nimehuzunika kwa sababu nilikuwa na kila sababu ya kuwa na furaha baada ya kuona dakika zinaendelea kuyoyoma tukiwa tunaongoza kwa bao la mapema.
“Licha ya kupata bao la mapema lakini vijana walicheza vizuri, leo hawakuwa kwenye fomu ya kawaida, walikuwa chini kidogo. Wenzetu walikuwa wachache sisi tuko wengi lakini hatukutumia pengo la huyo mtu mmoja.
“Lakini baadhi ya watu wamehuzunika na Watanzania wote wamehuzunika hata wachezaji wenyewe. Nadhani tuwape nafasi vijana.
“Mimi nilikuwa tofauti na watu waliokuwa wanawabeza wale jamaa, angalia walikuwa wachache lakini utaona wao walikuwa kama ndio wengi kwenye uwanja, pasi wanazopiga, mikimbio yao na mwisho wa siku wamepata bao wakapata sare,” amesema Julio.