Kuna vipenzi vya mashabiki na wanasubiriwa kwa hamu katika fainali za Kombe la Dunia zikiwa zimebaki wiki mbili tu.
Licha ya fainali hizi kushirikisha mataifa 32 mastaa hawa ndio wanakubalika zaidi kutokana na historia na viwango vyao bora akiwemo Lionel Messi na Cristiano Ronaldo ambao wametawajwa katika orodha.
1.Lionel Messi,
Argentina
Klabu: Paris Saint-Germain
Umri: 35
Nafasi: Winga
Messi ni mchezaji anayependwa na mashabiki duniani kutokana na ubora wake wa kucheza soka aliloonyesha tangu alipokuwa mdogo.
Nyoa huyo anayekipiga Paris Saint-Germain ameweka rekodi ya kubeba Tuzo za Ballon d’Or sita akimpiku Ronaldo.
Amebeba mataji mengi alipokuwa akikipiga Barcelona kabla ya kujiunga na PSG. Nahodha huyo wa Timu ya Taifa Argentina ana ndoto ya kubeba Kombe la Dunia kwani hajawahi katika historia yake. Messi amepania kufanya vizuri Qatar baada ya kuangukia pua katika fainali zilizofanyika mwaka 2014.
2.Cristiano Ronaldo, Ureno
Klabu: Man United
Umri: 37
Nafai: Fowadi
Ronaldo alikuwa na mchango mkubwa timu yake kufuzu fainali za Kombe la Dunia hatua ya makundi. Katika mechi sita alizocheza ameifungia Ureno mabao saba. Huenda fainali hizi zikawa za mwisho kama Messi ambaye ametangaza rasmi.
Ronaldo ameweka rekodi nyingi katika mechi za kimataifa ikiwemo ya ufungaji bora kwani amefunga mabao 117 katika mechi 189 alizolitumikia taifa lake. Licha ya kusuasua msimu huu mashabiki wanamsubiri akiwa na kikosi cha Ureno. Staa huyo amebeba tuzo tano za Ballon d’Or.
3.Kylian Mbappe - Ufaransa
klabu: Paris Saint Germain
Umri: 23
Nafasi: fowadi
Mbappe ni shujaa wa Timu ya Taifa ya Ufaransa katika fainali za Kombe la Dunia zilizofanyika mwaka 2018. Fowadi huyu aliweka rekodi ya mchezaji kinda aliyefunga bao katika fainali alipokuwa na umri wa miaka 18.
Mbappe ameichezea Ufaransa mechi 57 na kufunga mabao 27. Katika historia ya soka Ligue 1, Mbappe anashika nafasi ya 19 katika orodha ya wachezaji walifunga mabao mengi katika ligi hiyo.
4. Neymar Jr, Brazil
Klabu:PSG
Umri: 30
Nafasi:Fowadi
Nyota huyu ana njaa ya kupata mafanikio ya kubeba taji la Kombe la Dunia, kwa muda mrefu mashabiki wamevutiwa na aina ya uchezaji. Ni mchezaji muhimu katika kikosi cha Brazil na ansaubiriwa kwa hamu na mashabiki Qatar. Neymar amekuwa hatari msimu huu akicheza sambamba na Mbappe, Messi katika safu ya ushambuliaji.
5. Kevin De Bruyne, Ubelgiji
Klabu: Man City
Umri: 31
Nafasi: Kiungo
Kiungo huyo anayekipiga Man City ana kipaji cha kucheza soka na safari hii mashabiki watamshuhudia katika fainali za Kombe la Dunia katika kikosi cha Ubelgiji.
Ametoa mchango mkubwa kwa Man City na kwa mujibu wa wakala wake soka lake huenda akalimalizia katika Ligi ya Marekani. Ni mchezaji wa hali juu anayekubalika na mashabiki. De Bruyne alishika nafasi ya tatu katika kinyang’anyiro cha kuwania Tuzo ya Ballon d’Or ambayo mwaka huu ilibebwa na Karim Benzema.
6.Karim Benzema, Ufaransa
Klabu: Real Madrid
Umri: 34
Nafasi: Fowadi
Benzema amegusa mioyo ya mashabiki duniani baada ya kushinda Ballon d’Or mwezi huu kwani alistahili kutokana na mchango wake aliyoonyesha Real Madrid na timu yake ya taifa ya Ufaransa ambayo aliipa ubingwa wa Kombe la Dunia mwaka 2018.
Benzema alimaliza msimu uliopita kwa mafanikio akibeba mataji matatu. Vilevile aliibuka kuwa mfungaji bora wa La Liga na kuzoa tuzo tatu mfulilizo zilizoandaliwa na MARCA.
7.Sadio Mane,
Senegal
Klabu: Bayern Munich
Umri :30
Nafasi: Fowadi
Mane anakubalika na mshabiki kutokana na roho yake yan ukarimu anapokuwa nje ya uwanjani. Amekuwa na mchango mkubwa kwa taifa lake la Senegal hususan watu wasiokuwa na uwezo. Mane alikuwa kinara katika fainali za Kombe la Mataifa Afrika (AFCON) mwaka huu akiisaidia Senegal kubeba ubingwa mbele ya Misri.
Fowadi huyo amefunga mabao sita katika mechi 13 za Bundesliga msimu huu. Vilevile alishika nafasi ya pili katika kinyang’anyiro cha kuwania Tuzo ya Ballon d’Or mwaka huu.