Uongozi wa Mashujaa umesema licha ya kipindi kigumu wanachopitia kwa kukosa matokeo mazuri, lakini bado wanayo matumaini na kocha wao, Abdalah Mohamed ‘Baresi’ wakiamini atawafikisha wanapotaka
Baresi alijiunga na timu hiyo iliyopanda Ligi Kuu kwa mara ya kwanza mapema msimu huu, ambapo licha ya kuanza vyema ligi lakini kwa sasa hali imekuwa mbaya kutokana na matokeo waliyonayo.
Katika mechi 11 ilizocheza timu hiyo, imeshinda miwili, sare tatu na kupoteza sita na kuwa nafasi ya 15 kwa pointi tisa na kuongeza presha kwa mashabiki wake katika kukwepa kushuka daraja.
Mwenyekiti wa timu hiyo, Yahya Mgaya alisema pamoja na matokeo yasiyoridhisha lakini bado hawajafikiria kuachana na Baresi isipokuwa wanaendelea kushirikiana naye kubadili hali ilivyo.
Alisema uongozi unaendelea kuweka mipango ikiwamo hamasa kwa wachezaji ili kuanzia mechi zijazo dhidi ya Mbuga FC katika Kombe la Shirikisho la Azam na Mtibwa Sugar kuhakikisha wanashinda.
“Kila mmoja anaumizwa na matokeo haya lakini tunashirikiana kuondokana na maumivu haya. Uongozi unaweka mazingira mazuri lakini tukisubiri ripoti yake kwenye dirisha dogo kuona namna ya kuboresha kikosi.”