Mkuu wa Mkoa wa zamani wa Morogoro, Stephen Mashishanga amesema ili Tanzania iandike historia mpya kwa kuingiza timu mbili katika nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika ni lazima wadau wote nchini wawe na umoja.
Akizungumza na Mwanaspoti, Mashishanga alisema kwa kuwa timu zote zinatokea Tanzania hakuna haja ya kusapoti wageni ambao hawana faida kwa taifa.
Aliongeza kuwa ili kufanya vyema kwenye mechi za nyumbani ni vizuri mashabiki wa Tanzania kuweka utani kando na kupeana sapoti ili timu zetu zitimize ndoto ya taifa.
"Tulalie upande wa nchi yetu, ni vizuri wanapocheza Simba na Yanga tushangilie sote kwa pamoja, itawapa hofu hata wageni wanapokuja washangae uwanja umejaa na mnakuwa kitu kimoja ili timu zetu zote zishinde na kwenda nusu fainali," alisema Mashishanga.