Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mashabiki Yanga: Kwa kikosi hiki, tutawapiga mno

Yanga Kikosi 2024 25 Q.jpeg Mashabiki Yanga: Kwa kikosi hiki, tutawapiga mno

Mon, 5 Aug 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Kilele cha Wiki ya Mwananchi (Yanga Day) kilihitimishwa jana Agosti 4, katika Uwanja wa Benjamin Mkapa, jijini Dar es Salaam kwa klabu hiyo kutambulisha kikosi kipya cha wachezaji na benchi la ufundi.

Yanga Day ni siku maalum na klabu ya Yanga inakutanisha mashabiki wake kwa shamrashamra za aina yake huku ikiwatambulisha nyota wapya na benchi la ufundi watakaoiongoza msimu ujao, burudani kutoka kwa wasanii na mchezo wa kirafiki.

Wakati mzuka wa Wana Yanga nchini na nje ya nchi ukipanda, mashabiki wa timu hiyo jijini Mwanza nao walifanya maandalizi kabambe ya kushiriki tamasha hilo na kuipa nguvu timu yao.

Mjumbe wa kamati ya safari tawi la Yanga Mwanza Mjini, Avichi Bake, alisema msafara wa mashabiki zaidi ya 100 uliondoka jijini Mwanza kwenda jijini Dar es Salaam kuipa nguvu chama lao.

Alisema mashabiki 108 walilipa nauli ya Sh90,000 kwenda na kurudi jijini Dar es Salaam na watashuhudia tamasha hilo mchezo wa Ngao ya Jamii Agosti 8, mwaka huu dhidi ya watani wao, Simba katika Uwanja wa Benjamin Mkapa.

“Tunapata jeuri na hamasa hii kwa sababu jeshi letu kwa asilimia kubwa limebakizwa na tunaamini tutakuwa na mwendelezo wa msimu uliopita, timu yetu ni nzuri tumeiona katika mechi za kirafiki.

“Nawaambia mashabiki kwa kweli hawatajutia kwa sababu timu itawapa burudani, kikosi kinatosha kupambana na timu yoyote hapa Afrika, tunaomba wanachama wote wawahi na wajae uwanjani waitazame Yanga ikitoa burudani,” alisema.

Mwanachama wa Yanga jijini hapa, Getrude Macheda alisema kwa usajili uliofanyika msimu huu viongozi wao hawana deni kwa sababu wameleta wachezaji bora ili kuwapa raha mashabiki na wanachama wao.

“Sisi mashabiki na wanachama ndio tuna deni, tunatakiwa tuipe sapoti timu yetu, tulipie ada zetu tutambulike na klabu yetu tusiishie kupiga kelele barabarani na kubishana vijiwe vya kahawa, tuna timu nzuri, benchi na kikosi kizuri tuwaunge mkono tuwashangilie,” alisema Macheda.

“Nawaomba wanachama tujitokeze wiki ya Mwananchi tuishangilie kwa wingi, mashabiki wa Yanga kwa hizi raha tunazopata, imeleta hamasa kwa wanawake kupenda soka na kuvutiwa na timu yetu.”

“Nina matumaini makubwa sana ukiangalia kikosi chetu asilimia kubwa wachezaji wamebaki ili kufikia malengo tuliyojiwekea, nina imani na timu yangu, naamini tutafika mbali na kucheza fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu ujao. Ninaiamini klabu yangu, uongozi na wachezaji wetu,” alisema.

Msemaji wa tawi la Yanga Mwanza Mjini, Justin Kiseke alisema klabu yao ina wachezaji wanaoweza kuleta mafanikio na mataji ya aina yoyote wanayoyahitaji, huku akiwaomba wanachama na mashabiki kufurika kwenye kilele cha Wiki ya Mwananchi kupata burudani.

“Tuko vizuri kwenda kuiunga mkono timu yetu tuna matumaini na kikosi na viongozi wanaoipambania iendelee kufanya vizuri ndani na kimataifa. Wanachama ambao hawajajisajili hawaitendei haki klabu yetu kwa sababu tuna wachezaji wanaoweza kutupa kila kitu ambacho tunahitaji.”

“Yanga ni bingwa msimu ujao tunajiamini kwa sababu viongozi wamefanya kazi kubwa wametimiza majukumu yao na sisi wanachama lazima tuamke tuwaunge mkono na kuisapoti klabu kwa kwenda kuishangilia mahali popote ilipo,” alisema Kiseke na kuongeza;

“Sisi Yanga tumejipanga kuna timu zitafungwa mabao 10-0 ni kiama, kuna timu zitalalamika tunapanga matokeo nawatahadharisha wawe makini Yanga hii ni hatari. Yanga ni klabu ya kimataifa hatuwekezi kwenye propaganda kama wenzetu sisi tunawekeza kwenye utendaji kazi,” alisema.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live