Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Masau Bwire: Ruvu Shooting tunamuachia Mungu

Masau Bwire Afisa Habari wa Ruvu Shooting, Masau Bwire

Sun, 7 May 2023 Chanzo: Dar24

Uongozi wa Ruvu Shooting umeeleza kulingana na wapinzani wanaotarajia kukutana nao kwenye michezo yao mitatu iliyosalia ya Ligi Kuu Tanzania Bara, hawana pa kuegemea zaidi ya kumwachia Mungu awatetee.

Ruvu inayopambana isishuke daraja msimu huu, inaburuza mkia kwa alama zao 20 baada michezo 27 hadi sasa.

Afisa Habari wa Ruvu Shooting, Masau Bwire ameeleza katika michezo hiyo iliyosalia wataanza na Simba SC kisha Singida Big Stars na mwisho Dodoma Jiji akiamini hiyo yote ni michezo migumu kwao, hivyo pamoja na maandalizi waliyonayo lakini wanamtanguliza Mungu kuwaepusha na kikombe cha kushuka daraja kupitia michezo hiyo.

“Michezo iliyo mbele yetu tunayoitazama ni ya Simba SC, kwa hali tuliyonayo, nafasi tuliyopo na uwezo tulionao kisoka kikubwa zaidi kwa sasa ni kumtanguliza Mungu kwa maana ya maombi zaidi.”

“Simba SC tumewaona kwenye mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika, pamoja na kuondolewa lakini ubora wao tumeuona, ni moja ya timu bora Afrika kwa sasa, kwa hiyo ni mechi ngumu kwetu na ndio nikasema pamoja na maandalizi tuliyonayo lakini tumekuwa kama na wasiwasi kutokana na hali zetu hivyo Mungu pekee anaweza kutusaidia kwa sasa, tuongeze maombi,” amesema Bwire.

Masau amefafanua kuwa anafahamu Watanzania wengi wanavutiwa na soka la Ruvu Shooting, hivyo ni heri wakawasaidia katika maombi hayo ili wapate matokeo katika michezo hiyo na mwisho wasalie Ligi Kuu msimu ujao 2023/24.

Chanzo: Dar24