Timu tatu za Ligi Kuu ya soka ya Marekani(MLS)zinataka kumsajili Cristiano Ronaldo, ripoti zimesema.
Mchezaji huyo wa kimataifa wa Ureno mwenye umri wa miaka 37 huenda akarejea katika michuano ya Ligi ya Europa leo usiku lakini anatarajiwa kuondoka Old Trafford mkataba wake utakapokamilika 2023.
Ripoti hizo zimesema klabu za Los Angeles, LA Glaxy na Inter Miami zote zina nia kumsajili mshambuliaji huyo kwa uhamisho huru.
Huku uhusiano kati ya mchezaji huyo na klabu yake ya sasa ukiwa tayari unayumba, kuna uwezekano kwamba United inaweza kutumia nafasi hiyo kuokoa kiasi cha fedha.
United pia inaweza kuzuia mgogoro zaidi kwa kumruhusu Ronaldo kuondoka msimu huu wa baridi, jambo ambalo litaruhusu timu za MLS na yoyote inayovutiwa kufanya mchakato mapema wa kumsajili.
Ronaldo ni mmoja wa wachezaji wanaolipwa fedha nyingi zaidi barani ulaya akipokea mshahara wa pauni 515,385 sawa na shilingi bilioni 1.3 kwa wiki.