Wakati mashindano ya First League yakianza kupigwa Oktoba 21, kocha wa Mapinduzi Stars, Athumani Bilali ‘Bilo’ amesema kwa sasa anahitaji mechi nne za kukipima kikosi chake kisha baada ya hapo atakuwa tayari kwa ajili ya mashindano hayo.
Mapinduzi itacheza kwa mara ya kwanza mashindano hayo baada ya kupanda daraja ambapo imepangwa kundi B, wakiwa na timu za Alliance FC, Kurugenzi, Mwadui, TRA FC, Kasulu United, Tanesco na Rhino Rangers.
Klabu hiyo yenye maskani yake jijini Mwanza itaanza harakati zake kwenye mashindano hayo kwa kukipiga na Kurugenzi katika mchezo utakaochezwa Oktoba 21 Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga.
Bilo amesema kwa sasa wako katika maandalizi ya ligi hiyo ambapo kabla ya mashindano hayo kuanza ni lazima acheze mechi nne za kukipima kikosi chake na baada ya hapo watakuwa tayari kwa michuano hiyo.
Amesema katika mchanganuo wa timu watakazocheza nazo mechi hizo za kirafiki, watacheza na klabu tatu zinazoshiriki First League na moja ya Championship ambapo anaamini michezo hiyo itakuwa kipimo tosha cha kujua kasoro za kikosi chake.