Kocha Mkuu wa Simba, Didier Gomes, amesema itakuwa ngumu kumuweka benchi kipa Aishi Manula ndani ya kikosi chake kutokana na ubora ambao anazidi kuuonesha kila siku.
Ndani ya kikosi cha Simba, Manula anaunda safu ya makipa sambamba na Beno Kakolanya, Jeremiah Kisubi na Ally Salim.
Akizungumza na Spoti Xtra, Gomes amesema: “Manula ni golikipa mzuri, kwa sasa ni miongoni mwa magolikipa bora ndani ya Afrika, anajiamini na anazidi kuimarika kila siku.
“Nimemtazama akiwa na kikosi cha timu ya taifa, alikuwa bora sana na aliisaidia timu yake kushinda.
“Ndani ya Simba ni ngumu kumuweka benchi, yeye atabaki kuwa kipa namba moja wa timu lakini bado kuna nafasi ya makipa wengine kupata nafasi katika kikosi chetu. Yupo Kakolanya, Kisubi na Salim, wote wanazidi kuimarika kila siku.”