Mabosi wa Manchester United wamepata matumaini makubwa ya kumsajili kiungo wa Benfica na Ureno Joao Neves, 19, katika dirisha hili baada ya staa huyo kugoma kusaini mkataba mpya wa kuendelea kuitumikia timu hiyo.
Neves amekuwa akiwindwa na timu nyingi katika dirisha hili ikiwemo Man City na Benfica ilikuwa inataka kumuongeza mkataba ili imuuze kwa pesa nyingi zaidi.
Man United inahitaji huduma ya kiungo huyu ili akazibe pengo la Casemiro ambaye yupo kwenye rada za timu kutoka Saudi Arabia.
Katika siku chache zilizopita, mashetani hawa wekundu waliwasilisha ofa ya Pauni 51 milioni kwenda Benfica lakini ilikataliwa.
Kwa mujibu wa tovuti ya Metro, Neves mwenye umri wa miaka 19, ana kipengele kwenye mkataba wake ambacho kinairuhusu timu inayomhitaji kutoa Pauni 105 milioni ili kuipata saini yake jambo linaoonekana kuwa gumu kwa Man United inayotaka kutoa pungufu ya dau hilo.