Kazi bado inaendelea ndani ya Man United licha ya michezo 2 kughairishwa. United wanaendelea na maboresho ya benchi la ufundi na mfumo wa klabu nzima.
Imeripotiwa kuwa, Man United ipo mbioni kumtangaza Richard Arnord kama mkurugenzi mkuu wa klabu hiyo baada ya Ed Woodward kuachia nafasi hiyo. Arnord anakwenda kuchukua nafasi ambayo haikuwahi kuzibwa toka 2013 alivyoondoka David Gill.
Pamoja na uongozi katika ngazi za juu, United ipo mbioni kumpatia nafasi Ewan Sharp kwenye benchi la ufundi la timu hiyo. Kocha wa sasa, Ralf Rangnick, anashughulikia mchakato huo ambao unatarajiwa kukamilika ndani ya siku chache zijazo.
Sharp atajiunga na United akitokea Lokomotiv Moscow ambapo alikuwa akifanya kazi na Rangnick hapo awali. Wawili hawa walikutana New York Red Bulls wakati ule, Ewan alikua mchambuzi kwenye klabu hiyo.
Wasifu wa Ewan unaonesha kuwa, aliwahi kuwa kocha wa Toronto FC ambapo alifanya kazi na Chris Amas kwa miezi 6 kabla ya Amas kufukuzwa klabuni hapo. Sasa hivi, wawili hawa wanakwenda kukutana tena Man United wakiwa chini ya Ralf Rangnick na Mike Phelan.