Makomandoo wa Yanga wamejitokeza kwa wingi katika msafara wa timu hiyo katika kuhitimisha gwaride la heshima la kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Bara kwa msimu wa pili mfululizo.
Katika msafara wa gari iliyobeba wachezaji, Makomandoo hao wanaodaiwa wa Yanga wamekuwa bega kwa bega huku wakiizunguka pande zote kwa ajili ya usalama.
Gari hiyo ambayo imeandaliwa maalumu kwa ajili ya gwaride hilo, Makomandoo hao wamekuwa wakitembea kwa miguu huku wakilinda usalama wa wachezaji waliokuwa ndani.
Yanga imekuwa na mafanikio katika msimu huu kwani mbali na kuchukua ubingwa ila imefika fainali ya Kombe la Shirikisho la Afrika ambapo ilitolewa kwa bao la ugenini na USM Alger ya Algeria baada ya timu hizo kufungana mabao 2-2.
Licha ya hivyo ila pia Yanga imebakiwa na fainali moja ya Kombe la Shirikisho la Azam (ASFC) ambapo itacheza na Azam siku ya Jumatatu kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.