Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mafuriko yaathiri 200 Segerea, waomba kuharakishwa ujenzi Mto Msimbazi

Mafuriko Yaathiri 200 Segerea Mafuriko yaathiri 200 Segerea, waomba kuharakishwa ujenzi Mto Msimbazi

Thu, 16 Nov 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Zaidi ya wakazi 200 wa Jimbo la Segerea wameathiriwa na mafuriko kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha na kuiomba Serikali kuharakisha ujenzi wa kingo za Mto Msimbazi ili kuwanusuru.

Mbunge wa Segerea, Bonnah Kamoli, jana Novemba 15,2023 amefanya ziara kuangalia athari zilizotokana na mafuriko na kuwapa pole wananchi walioathiriwa katika Kata za Kipawa, Bonyokwa, Vingunguti, Mnyamani na Liwiti.

Amesema ingawa bonde hilo liko kwenye mkakati wa kujenga ameiomba Serikali kuharakisha ujenzi huo hasa katika maeneo yaliyoathiriwa ili kuepusha athari zaidi zisitokee.

Mbunge wa Segerea, Bonnah Kamoli, akipita kando ya Mto Msimbazi alipokwenda kuwapa pole wananchi walioathiriwa na mafuriko katika Mtaa wa Mfaume Kata ya Liwiti, Dar es Salaam.

“Bonde la Mto Msimbazi limekuwa ni kikwazo kikubwa kwa wananchi wetu, maji yanawafuata wananchi kutokana na miundombinu mibovu, wakandarasi waaanzie sehemu ambazo watu wako karibu na bonde kama vile Mnyamani, Kipawa, Liwiti na Tabata,” amesema Kamoli.

Kwa mujibu wa mbunge huyo katika Kata ya Mnyamani watu 94 wameathiriwa wakati katika Kata ya Kipawa pia ni 74 na Liwiti ni 69.

Mbunge wa Segerea, Bonnah Kamoli, akiangalia athari zilizotokana na mvua zinazoendelea kunyesha katika Kata ya Mnyamani, Dar es Salaam.

Diwani wa Kata ya Kipawa, Aidan Kwezi, amesema kaya 74 hazina mahala pa kukaa na nyingine zina changamoto za kukosa huduma muhimu za kibinadamu kama chakula na nyingine.

Aidha amesema mvua zitakapopungua watahakikisha gema la mchanga lililoko katika mto huo linaondolewa ili kuendelea kudhibiti eneo hilo lizisidi kuathiriwa.

“Tuna nguzo kubwa ya umeme imebakia mita chache kufikiwa hivyo, inabidi tuweke nguvu za ziada kuhakikisha tunasogeza mto mbali ili nyumba na miundombinu ya umeme isiathiriwe,” amesema Kwezi.

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Ilala, Saidi Sidde, amesema; “Kila mwaka Mto Msimbazi umekuwa na athari sana, Wilaya ya Ilala imeathirika kwa kiasi kikubwa na mafuriko yanayotokana na Mto Msimbazi, tunaiomba Serikali iharakishe ujenzi ili wananchi wasiendelee kupata athari,” amesema Sidde.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live