Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

MGUU NDANI, MGUU NJE…Hawa kutua Saudia ni suala la muda tu

Mguu Ndani X Mguu Nje MGUU NDANI, MGUU NJE…Hawa kutua Saudia ni suala la muda tu

Sun, 28 Jul 2024 Chanzo: Mwanaspoti

Dirisha la usajili bado linaendelea na timu zinazidi kusajili kila kukicha. Miongoni mwa timu ambazo usajili wake huwa unatikisa ni zile za Saudi Arabia ambazo zimekuwa zikichukua wachezaji bora kutoka timu mbalimbali Ulaya.

Kwa sasa kuna zaidi ya wachezaji 10 kutoka timu mbalimbali kubwa Ulaya na muda wowote wanaweza kutua Saudi Arabia.

Baadhi ya mastaa walianza kuwindwa dirisha la majira ya kiangazi mwaka jana na ilishindikana kuwapata na sasa Waarabu wakarudi tena na muda wowote wanaweza kukamilisha madili ya kuwasajili. Hawa hapa wachezaji 10 kutoka England wanaoweza kusajiliwa na timu za Saudi Arabia muda wowote katika dirisha hili.

Gabriel Jesus

Amekuwa akisumbuliwa na majeraha ya mara kwa mara yanayomweka nje ya uwanja kwa muda mrefu na hali hiyo inadaiwa kuwafanya Arsenal kuwa tayari kumuuza dirisha hili ili kutumia pesa zake kwa ajili ya kusajili mshambuliaji mwingine.

Jesus anawindwa na Al-Ahli inayohitaji saini yake dirisha hili na ikiwa atakamilisha dili hilo ataenda kuungana na mchezaji mwenzake wa zamani wa Manchester City, Riyad Mahrez.

Kwa sasa amebakiza miaka mitatu katika mkataba wake lakini inaelezwa Arsenal ipo tayari kumuuza.

Richarlison

Jesus sio mshambuliaji pekee wa Brazil ambaye Al-Ahli inamtaka, pia inahitaji huduma ya straika wa Tottenham, Richarlison.

Nyota huyo wa zamani wa Everton na Watford licha ya kucheza mara kwa mara, mchango wake katika ufungaji ni hafifu na katika misimu miwili iliyopita alifunga mabao 15 tu Ligi Kuu England.

Ripoti za hapo awali zilidai staa huyu anahitajika na Al-Hilal lakini alikanusha kupitia ukurasa wake wa Instagram taarifa hizo ni za uongo.

Kevin De Bruyne

Hivi karibuni tetesi za kiungo huyu kutua Saudi Arabia ndizo zilishika vichwa vya habari duniani na hadi sasa haijafahamika ikiwa ataondoka ama atabaki.

Mchezaji huyo wa Manchester City na timu ya taifa ya Ubelgiji amebakiza mwaka mmoja tu kwenye mkataba wake na hapo awali aliwahi kusema yuko tayari kuhamia Saudi.

Siku kadhaa zilizopita, alielezwa amefanya makubaliano binafsi ya kujiunga na Al-Ittihad na kilichobakia ni timu hiyo kufanya mazungumzo na Manchester City ili kukubaliana kuhusu ada ya usajili.

Ikiwa De Bruyne atajiunga na timu hii, ataungana na Karim Benzema, Houssem Aouar, Fabinho na N’Golo Kante.

Ederson

Katika kikosi cha Manchester City sio De Bruyne pekee anayehusishwa na timu hizi za Saudi Arabia, kwa mujibu wa ripoti Al-Ittihad pia inamvizia mchezaji mwenzake Ederson.

Inaelezwa Ederson yupo tayari kujiunga na Waarabu hao lakini changamoto ipo kwa Man City iliyokataa ofa ya Pauni 25 milioni kutoka Ittihad.

Hata hivyo, hivi karibuni Man City imekuwa ikihusishwa kutaka kumsajili kipa wa PSG, Gianluigi Donnarumma hali inayotoa ishara inaweza kumwachia Ederson.

Alisson Becker

Ripoti zinaeleza wawakilishi wa kipa huyu wamefanya mazungumzo na Al-Nassr ili Becker atue hapo na timu hiyo inajaribu kumtumia staa wao Sadio Mane kumshawishi akubali kujiunga nao dirisha hili.

Alisson mwenye umri wa miaka 31, amebakiza miaka mitatu kwenye mkataba wake na kocha mpya Arne Slot amesisitiza bado anahitaji huduma yake lakini mambo yanaweza kubadilika ikiwa Al Nassr itaweka pesa nyingi zaidi na kipa huyo akalazimisha kuondoka.

Mohamed Salah

Huyu amekuwa mmoja wa wachezaji maarufu wanaotajwa kutua Saudi Arabia tangu mwaka jana.

Ripoti zinaeleza Salah anataka kuondoka Liverpool dirisha hili na timu pekee anayoweza kujiunga nayo ni Al Ittihad ambayo mwaka jana dirisha la majira ya kiangazi iliwasilisha ofa ya Pauni 150 milioni ili kumsajili lakini ilikataliwa.

Salah amebakiza mwaka mmoja katika mkataba wake na mabosi wa Liverpool wanajaribu kufanya naye mazungumzo lakini ikishindikana wanaweza kumuuza ili asiondoke bure mwisho wa msimu ujao.

Casemiro

Licha ya kuwa na msimu wa kwanza wa kuvutia Old Trafford, mambo hayakwenda vizuri sana msimu uliopita na anatajwa kuwa mmoja wa mastaa saba ambao Man United inataka kuwauza dirisha hili.

Amekuwa akitajwa huenda akatua Al-Nassr au Al-Ittihad dirisha hili.

Man United inahitaji walau Pauni 30 milioni ili kumwachia Casemiro ambaye amebakiza miaka miwili katika mkataba wake.

Kepa Arrizabalaga

Bado anaendelea kushikilia rekodi ya kuwa kipa ghali zaidi duniani kutokana na usajili wake wa Euro 80 milioni aliokamilisha mwaka 2018 akitokea Athletic Bilbao kutua Chelsea.

Hadi sasa hatma yake katika kikosi cha Chelsea bado haijajulikana huku akiwa ameachwa katika kikosi cha timu hiyo kilichokita kambi huko Marekani kwa ajili ya maandalizi ya msimu mpya.

Kwa sasa Robert Sanchez ndiye namba moja wa matajiri hao wa London na taarifa za ndani zinaeleza Kepa ambaye msimu uliopita alicheza kwa mkopo Real Madrid, amepewa ruhusa ya kuondoka ikiwa atapata timu itakayokuwa tayari kumnunua kwa pesa inayohitajika na Chelsea.

Timu anayohusishwa nayo kwa sasa ni Al-Ittihad ambayo inamtafuta baada ya kushindwa kuwanasa Ederson na Allison Becker.

Lucas Paqueta

Baada ya kushtakiwa kwa kukiuka sheria za kamari za FA, kiungo wa raia wa Brazil, Paqueta amehusishwa na kuondoka West Ham tangu kuanza kwa dirisha hili.

Flamengo wamejaribu kumsajili lakini dili hilo linaonekana kuwa gumu kufanyika kutokana na pesa nyingi anazohitaji staa huyo.

Timu ya Saudia inayohusishwa naye ni Al-Nassr ingawa hakuna taarifa kamili kama wameshaanza mazungumzo au la.

Paqueta, 26, ameichezea West Ham mechi 84 tangu alipojiunga nayo akitokea Olympique Lyon miaka miwili iliyopita.

Callum Wilson

Staa huyu wa zamani wa Bournemouth alifunga mabao 10 katika michuano yote msimu uliopita na hakupata muda mwingi wa kucheza kutokana na majeraha.

Amebakiza mwaka mmoja tu kwenye mkataba wake na ripoti zinadai ni miongoni mwa wachezaji ambao Arsenal inataka kuwauza dirisha hili.

Al-Fateh na Al-Ahli ni miongoni mwa timu kutoka Saudia zizazotajwa kutaka kumsajili na zote zimeshaanza mazungumzo na wawakilishi wake.

Chanzo: Mwanaspoti