TUNASHUKURU tumefika salama Sudan baada ya safari ndefu kutoka jijini Dar es Salaam kwa ajili ya mchezo wetu wa tatu wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya wenyeji wetu, Al Merreikh.
Mchezo huu utapigwa Jumamosi (kesho) na kwa hakika lazima nikiri, tutakuwa na mechi ngumu kuliko mbili tulizocheza dhidi ya AS Vita ya DR Congo na Al Ahly ya Misri, tofauti na wengi wanavyouchukulia mchezo huo.
Kama mchezaji huwa najua namna inavyokuwa unapokabiliana na timu iliyopoteza michezo miwili mfululizo. Al Merreikh ilipoteza mechi zao za awali katika hatua hii ya makundi na hii ndio inayoufanya mchezo huu kuwa mgumu.
Wapinzani wetu wamepoteza mechi ya kwanza ugenini dhidi ya Al Ahly ambayo ni timu kubwa na jambo hilo halina kubishi.
Baada ya hapo walirudi nyumbani kwao kucheza na Vita wakapoteza kwa mara nyingine, hivyo ni wazi hawatakubali kufungwa tena nyumbani kirahisi.
Wakati wao hawatakubali kufungwa nyumbani, wanakutana na Simba ambayo mechi zetu mbili za awali tumeshinda.