STRAIKA wa zamani wa Yanga na Taifa Stars, Edbily Lunyamila amesema aliyekuwa Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Hayati John Pombe Magufuli ameacha alama kila kona, zitakazotoa funzo la kupambana na kuwa mfano dhidi ya mataifa mengine.
Lunyamila ameliambia Mwanaspoti online, leo Jumamosi ya Machi 20, 2021 kwamba Hayati Magufuli alikuwa mchapakazi na alitaka kila Mtanzania ajitume katika nafasi aliopo ili kujenga Tanzania imara kila sekta. "Alikuwa mchapakazi kwa vitendo na alisisitiza kitakachotukwamua kutoka sehemu moja kwenda nyingine ni kufanya kazi kwa bidii, amefanya mambo mengi ya wazi ambayo hata vizazi vitakavyokuja vitaona alama yake," amesema na ameongeza kuwa;
"Katika michezo nako alitamani mataji ya Afrika yatue Tanzania, alisisitiza kufanya kazi kwa umakini na juhudi, kiukweli alikuwa ni Rais wa baraka, inaumiza sana lakini Mungu ndiye aliyetupa zawadi ya maisha yake na ameamua kumpumzisha kwa amani,"amesema.
Amesema Hayati Magufuli anatakiwa kuenziwa kwa kuendeleza misingi imara ya utendaji kazi wake ambao ulianza kutoa taswira ya kuwa na Tanzania imara kwa kila sekta, ikiwemo ya wanamichezo ambao walimulikwa kwa jicho makini.