Klabu ya Liverpool imejiondoa katika mbio za kuinasa saini ya kocha wa Bayer Leverkusen, Xabi Alonso aliyetajwa kuhitajika kuchukua mikoba ya Jurgen Klopp anayejiandaa kuondoka klabuni hapo mwishoni mwa msimu.
Hatua hiyo imekuja baada ya Liverpool kuona nafasi finyu ya kumng’oa Alonso Leverkusen kwani wanaamini hatahitaji sana kuondoka klabuni hapo kufuatia makubaliano na mradi unaojengwa ndani ya timu hiyo.
Kiungo huyo wa zamani wa Liverpool ameripotiwa kujumuishwa kwenye mipango ya usajili ya Leverkusen kwa msimu ujao huku akiripotiwa kushinikiza wachezaji wake nyota kama Florian Wirtz kubaki.
Mbali na Liverpool, vilabu vya Bayern Munich na Real Madrid pia vinafuatulia kwa karibu mustakabali wa kocha huyo ambaye mkataba wake unafika ukomo mwaka 2025.