Majogoo wa Jiji, Klabu ya Liverpool wameichapa Manchester City magoli 3-1 na kufanikiwa kutwaa Kombe la ngao ya Jamii katika mchezo uliopigwa katika Uwanja wa King Power.
Mchezo huo uliovuta hisia za wengi ulikuwa wa kasi na Liverpool ndio waliokuwa wa kwanza kuanza kupata goli kipindi cha kwanza likiwekwa wavuni na Trent- Alexander Arnold dakika ya 21.
Mpaka dakika 45 za Kipindi cha kwanza zinakamilika Liver walikuwa mbele kwa uonngozi wa goli 1-0.
Kipindi cha pili Manchester City walirudi kwa kasi na kufanya mabadiliko yaliyowapa nguvu ya kusawazisha goli kupitia kwa Alvarez dakika ya 70.
Liverpool walipata penati dakika chache mbele baada ya beki Ruben Diaz kunawa mpira wa kichwa uliopigwa na Darwin Nunez.
Mohammed Salah akaandika bao la pili kwa mkwaju wa Penati na dakika za lala salama Darwin Nunez akaiandikia Liverpool bao la tatu na mpaka dakika 90 zinakamilika Liverpool akaibuka na ushindi wa magoli 3-1.
Kombe hilo la kuashiria ufunguzi wa Ligi Kuu England (EPL) linamfanya Kocha Jurgen Klopp kuandika rekodi ya kubeba kila aina ya kikombe kwa ngazi ya Klabu akiwa na Liverpool.
Klopp amebeba taji la EPL, UEFA, Klabu Bingwa ya Dunia, UEFA Super Cup, Carabao Cup, FA Cup, na leo ameiwezesha Liver kubeba taji la Ngao ya Jamii.