Licha ya Simba SC kumtambulisha beki, Lameck Lawi jana jioni, usiku wa jana hiyo hiyo viongozi wa Coastal Union wamesema wao wanatambua kuwa Lameck Lawi bado ni mchezaji wao halali na watamtumia msimu ujao.
"Ni kweli tulikuwa na mawasiliano na Simba lakini walishindwa kufikia ofa tuliyotaka. Lameck Lawi ni moja ya nguzo muhimu kwenye timu yetu hivyo hatuna mpango wa kumuuza tutamtumia msimu ujao.
"Siku hizi mitandaoni kuna mambo mengi sana wakati mwingine kuna mambo ya kufurahisha na kuchekesha.
"Hata sisi hizo taarifa tumeziona mitandaoni na kuzua taharuki kwa mashabiki wetu, tunawaomba mashabiki watulie, Lawi ni mchezaji wa Coastal Union hatufikirii kumuuza. Kwa sasa yuko mapumzikoni.
“Ilipokuja ofa [Kutoka Simba] tuliwapa taratibu za kufuata na namna ya kufanya kama wanamuhitaji Lameck Lawi.
"Sasa sijui ni nini kimewafanya wasifanye vile sisi tunataka kwa hiyo na sisi baada ya kuona pengine hawana nia tena tukakaa na kuamua mengine.” amesema Abbas El Sabri Wamba, Msemaji wa Coastal Union Via Clouds fm.