NAMBA huwa hazidanganyi buana. Hata kama mechi za kirafiki za kutesti mitambo sio kigezo, lakini kwa nyota wapya sita waliosajiliwa na Yanga msimu huu wote wakiwa wa kigeni ni wazi, watani zao Simba lazima wajipange kama wanataka heshima yao idumu.
Ndio, kama hujui ni kwamba tangu Februari 20, mwaka 2016 Yanga iliposhinda mabao 2-0 dhidi ya Simba katika pambano la watani, timu hiyo haijaonja raha yoyote tena kwa wapinzani wao hao, sanasana ni vipigo ama kuambulia sare.
Hata hivyo mashabiki wa Yanga wamekuwa na kelele nyingi mitaani kwa sasa wakitambia jeshi lililosajiliwa Jangwani, Simba wajipange maumivu na hii ikitokana na matokeo ya mechi za kutesti mitambo majembe yao mapya walivyofanya vurugu ya kutupia nyavuni.
Yanga iliyokuwa imejichimbia kambini mjini Morogoro ambapo asubuhii walikuwa wakifanya tizi la mwisho kabla ya kupakia mizigo yao kurudi jijini Dar es Salaam mchana kujiandaa na Tamasha la Wiki ya Mwananchi itakayofanyika Jumapili hii.
Katika mechi zao sita buana Yanga imefanikiwa kushinda zote na kukusanya mabao 25, huku wavu wao ukiguswa mara moja, huku nyota wake wa kigeni wa safu ya mbele wakizalisha mabao 14 wakiwafunika wenzao wapya wa Msimbazi ambao licha ya kucheza mechi nne nchini Afrika Kusini, wameshinda mbili na kutoka sare mbili.
Katika mechi hizo Simba ilifunga jumla ya mabao 10 na kufungwa matatu huku nyota wapya wawili tu ndio waliofunga mabao, akiwamo Mbrazili Wilker Da Silva na kiungo Shiboub Sharraf Eldin, na yaliyosaliwa yaliwekwa kambani na nyota waliokuwapo msimu uliopita kwa maana ya Meddie Kagere na Clatous Chama, John Bocco, Mzamiru Yasin na Hassan Dilunga nduio waliotupia kambani kuonyesha safu ya Yanga ni wembe ile mbaya.
Rekodi zinaonyesha kwenye mabao hayo 25 iliyozalisha Yanga katika mechi zake sita, Patrick Sibomana anaongoza kwa kufunga akitupia kambani mara 6, huku Juma Balinya akifunga manne, wakati Sadney Urikhob akifunga matatu na Issa Bigirimana akifunga moja sawa na beki Lamine Moro, huku na kiungo Mapinduzi Balama akifunga mawili.
Nyota wapya wa Yanga wamezalisha mabao 17, huku nane yaliyosalia yamefungwa na nyota waliokuwapo kikosi tangu msimu uliopita, Mrisho Ngassa akifunga matatu, Papy Tshishimbi mawili na viungo Rafael Daud na Feisal Salum kila mmoja akifunga bao moja.
Kwa upande wa Simba kwenye mechi zao nne Clatous Chama ndiye kinara akifunga mara tatu, akifuatiwa na nahodha John Bocco aliyefunga mawili, huku Meddie Kagere, Mzamiru Yasin na Hassani Dilunga kila mmoja akifunga bao moja sawa na wageni Wilker Da Silva na Shiboub Sharraf Eldin ambaye ni kiungo mpya kutoka Sudan.
Kwa picha lilivyoanza kwa vikosi vyote ambavyo vitakuwa na mechi za kutambulisha vikosi jijini Dar es Salaam dhidi ya timu kutoka nje ya nchi ni wazi kila timu inapaswa kujipanga, Simba ipange mabeki wake kuweza kuuzuia moto wa Yanga wakikutana.
Yanga itavaana na Kariobang Sharks ya Kenya Jumapili hii kwenye hitimisho la Wiki ya Mwananchi, wakati watani zao wataumana na Power Dynamo ya Zambia katika Kilele cha Simba Day kitakachofanyika Jumanne ijayo kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Wakati Simba ikitakiwa kujipanga hivyo, hatya Yanga nao kama hawajapata dawa ya kuwazuia kina Chama, Bocco na Kagere aliyewaliza kwenye mchezo wao wa mwisho katika msimu uliopita, basi nao wataumia kwa vile inaonekena moto wa nyota hao haujapoa kabisa.
Chini ni rekodi za mechi za kirafiki za Simba na Yanga na wafungaji wake;
YANGA MOTO
Julai 15, 2019
Yanga 10-1 Tanzanite FC (kirafiki, Highlands Park Morogoro)
Wafungaji;
Sibomana, Bigirimana, Tshishimbi, Balama, Balinya, Ngassa (3), Rafael na Fei Toto
Julai 18, 2019
Yanga 2-0 Moro Kids (kirafiki, Highlands Park, Moro)
Wafungaji;
Balinya (pen), Paul Godfrey 'Boxer'.
Julai 23, 2019
Yanga 7-0 ATN Academy (Kirafiki, Highlands Park, Moro)
Wafungaji:
Sibomana (3), Urikhob (2), Balinya na Lamine Moro
Julai 27, 2019
Yanga 3-0 Moro Combaine (Kirafiki, Highlands Park, Moro)
Wafungaji:
Juma Balinya, Patrick Sibomana na Balama Mapinduzi
Julai 28, 2019
Yanga 1-0 Mawenzi Market (Kirafiki Jamhuri, Moro)
Wafungaji:
Patrick Sibomana
Julai 30, 2019
Yanga 2-0 Friends Ranger (Kirafiki, Jamhuri, Moro)
Wafungaji:
Sadney Urikhob, Papy Tshishimbi
SIMBA NAKO HATARI
Julai 23, 2019
Simba 4-0 Orbit Tvet (kirafiki, Rosternburg, SA)
Wafungaji:
John Bocco (2), Hassan Dilunga na Wilker Da Silva
Julai 25, 2019
Simba 4-1 Platnum Stars (kirafiki, Rosternburg, SA)
Wafungaji:
Clatous Chama (2), Shiboub Sharraf Eldin na Mzamiru Yassin
Julai 27, 2019
Simba 1-1 Township Rollers (kirafiki, Rosternburg, SA)
Wafungaji:
Meddie Kagere
Julai 30, 2019
Simba 1-1 Orlando Pirates (KIrafiki, Rand Stadium, Johannesburg, SA)
Wafungaji:
Clatous Chama