BINGWA mtetezi wa Kombe la Shirikisho la Azam (ASFC), Simba itacheza na Dodoma Jiji katika mchezo wa Robo fainali kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
Katika droo iliyochezwa jana kwenye kituo cha runinga cha Azam ikisimamiwa na Meneja Mashindano wa Shirikisho la Mpira wa Miguu (TFF), Baraka Kizuguto alisema mechi za robo fainali zitachezwa kati ya Mei 25-28.
Robo fainali ya pili itakuwa kati ya Biashara United na Namungo FC katika Uwanja wa Karume, Mara, Rhino Rangers itaikaribisha Azam FC kwenye Uwanja wa CCM Kambarage, Shinyanga na Mwadui FC itakuwa mgeni wa Yanga.
Kwa mujibu wa droo hiyo mchezo wa nusu fainali ya kwanza utakuwa kati ya mshindi wa mchezo wa Rhino Rengers na Azam FC na mshindi wa mchezo wa Simba na Dodoma Jiji.
Nusu fainali ya pili itazikutanisha timu zitakazoshinda katika mchezo wa Biashara United na Namungo FC dhidi ya mshindi wa mchezo wa Mwadui FC na Yanga.
Nusu fainali zinatarajiwa kuchezwa kati ya Juni kati kati na Julai mwanzoni katika viwanja vya Ali Hassan Mwinyi Tabora na Majimaji Songea na fainali inatarajiwa kuchezwa Julai 18 katika Uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma.
Bingwa wa mashindano hayo atawakilisha nchi katika Mashindano ya Kombe la Shirikisho Afrika msimu ujao.