Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kufuzu Kombe la Dunia 2022 Taifa stars ilikwama hapa

Taifa Stars Stars yashindwa kufuzu Kombe la Dunia 2022

Sun, 14 Nov 2021 Chanzo: globalpublishers.co.tz

Kikosi cha Timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars, leo Jumapili kitahitimisha safari yake ya kucheza mechi za kufuzu Kombe la Dunia 2022 kwa kupambana na Madagascar.

Mchezo huo wa Kundi J, ni wa kukamilisha ratiba tu kwani timu hizo zote hazina nafasi ya kusonga mbele hata kama moja ikishinda leo.Msimamo wa Kundi J, unaonesha vinara ni Benin wenye pointi kumi, wakifuatiwa na DR Congo (8), Tanzania (7) na Madagascar (3), huku timu zote zikicheza mechi tano.

Kipigo cha mabao 0-3 nyumbani ambacho Taifa Stars walikipata Alhamisi wiki hii, ndicho kilizima kabisa ndoto za kufuzu Kombe la Dunia 2022, michuano itakayofanyika Qatar.

Kabla ya hapo, Taifa Stars ilionekana kuwa na nafasi ya kutinga hatua inayofuata ambayo ndiyo ilikuwa ya mwisho kabla ya kwenda Qatar.

Baada ya mechi nne kuchezwa kwa timu zote, Taifa Stars ilikuwa ikiongoza Kundi J ikikusanya pointi saba sawa na Benin, kilichokuwa kikiwatengenanisha ni idadi ya mabao ya kufunga.

Taifa Stars ilikuwa na matano na Benin matatu.Lakini sasa, Benin baada ya kuifunga Madagascar mabao 2-0, huku Taifa Stars ikifungwa 0-3, msimamo umebadilika na nafasi iliyobaki ni kwa Benin na DR Congo ambazo zitapambana leo kule DR Congo.

Baada ya Taifa Stars kufutiwa ndoto zao za kwenda Qatar, kila mmoja anazungumza lake kwa namna anavyofahamu, lakini kubwa zaidi ambalo linaonekana ni kitendo cha kushindwa kutumia vema uwanja wa nyumbani.

Katika mechi tano ambazo Taifa Stars imecheza mpaka sasa, tatu imecheza nyumbani na kujikuta ikikusanya pointi tatu pekee kwa kuifunga Madagascar 3-2.

Mechi mbili imepoteza nyumbani dhidi ya Benin (0-1) na DR Congo (0-3).Ukiangalia katika mechi hizo tatu, timu haikuwa vizuri kwenye kulinda lango lake kwani imeruhusu mabao sita, huku ikifunga matatu. Tofauti ya mabao ni -3.Ugenini, Taifa Stars ikiwa imecheza mechi mbili, imekusanya pointi nne, imeshinda (0-1) dhidi ya Benin na sare ya 1-1 dhidi ya DR Congo.

Kwa takwimu hizo, inaonekana Taifa Stars ugenini ipo vizuri kuliko nyumbani, lakini shida inakuwa kwenye kufunga mabao.

Katika mechi za namna hii ambazo zinachezwa ugenini na nyumbani, siku zote timu inayotumia vizuri uwanja wake wa nyumbani ndiyo huwa na nafasi kubwa ya kufanya vizuri.

Inaaminika kwamba, ugenini timu nyingi zinapokwenda kucheza hukutana na vikwazo vingi vinavyosababisha kuwa na nafasi ndogo ya kupata ushindi, lakini nyumbani, sehemu ambayo mazingira yote unayajua, ukipoteza unaonekana haupo makini.

Ndicho kilichoifelisha Taifa Stars.Ukiangalia Benin, vinara wa Kundi J, mechi zao tano walizocheza, tatu za nyumbani wameshinda moja, sare moja na kupoteza moja.

Ugenini imeshinda mbili, leo wanacheza ya tatu ugenini.DR Congo wao mechi mbili za nyumbani, wameshinda moja na sare moja, leo wanacheza ya tatu dhidi ya Benin.

Lakini ugenini wameshinda moja, sare moja na kupoteza moja.Madagascar nao ambao ni vibonde wa kundi, leo ni mechi yao ya tatu nyumbani dhidi ya Taifa Stars, lakini mbili zilizopita, wameshinda moja na kupoteza moja. Yaani hapa wametufunika hadi sisi.

Ugenini wamepoteza zote tatu.Zile mechi mbili dhidi ya DR Congo na Benin, kama Taifa Stars ingekuwa makini, leo hii tusingekuwa tunazungumza haya, lakini acha tujifunze, wakati mwingine tutakuwa makini zaidi.

KAULI YA KIM POULSEN

Kuelekea mchezo wa leo wa kukamilisha ratiba, Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Kim Poulsen anasema: “Hata kama hatuna nafasi ya kufuzu, haina maana tutaenda kuruhusu kufungwa, tutaenda kupambana hadi tone letu la mwisho.”

Chanzo: globalpublishers.co.tz