Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kombe la Shirikisho kufutwa, CAF yataja sababu

Yanga ZtR.jpeg Kombe la Shirikisho kufutwa, CAF yataja sababu

Sun, 14 Jan 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF), Patrice Motsepe amesema kuna uwezekano mkubwa wa mashindano ya Kombe la Shirikisho Afrika kufutwa kwa vile hayana faida kwa timu na mpira wa Afrika.

Akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari jijini Abidjan, Ivory Coast kunakofanyika fainali za Mataifa ya Afrika (Afcon), Motsepe alisema uamuzi huo unalenga kuyapa nguvu mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika na Kombe la Ligi ya Afrika (AFL) ambayo yana manufaa makubwa zaidi kwa klabu.

Motsepe alisema kuwa gharama za uendeshaji na usimamizi wa mpira wa miguu ni kubwa hivyo ni vyema kubaki na mashindano machache yenye ufanisi na faida hivyo CAF inajiandaa kufuta Kombe la Shirikisho Afrika.

"Nahitaji kupata fedha kwa ajili ya nchi wanachama, tunahitaji fedha kwa ajili ha maendeleo na kuongeza zawadi kwa washindi katika mashindano. Al Ahly, Wydad na klabu kwenye Ligi ya Mabingwa hazipati fedha, zinapoteza fedha.

"Hivyo tunataka Ligi ya Mabingwa Afrika na AFL kuwa na nguvu kubwa ya kiuchumi na kufanya klabu zitengeneze fedha lakini kitu kingine cha msingi ni tunaweza kufuta Kombe la Shirikisho. Hatuwezi kuwa na mashindano mengi," alisema Motsepe.

Ikiwa litafutwa, Kombe la Shirikisho Afrika litakuwa limedumu kwa muda wa miaka 21 tu kwani lilianza kwa mara ya kwanza mwaka 2023 baada ya kuunganishwa kwa mashindano ya Kombe la CAF na Kombe la washindi Afrika.

Kumbukumbu nzuri kwa timu ya Tanzania katika Kombe la Shirikisho Afrika ni msimu uliopita ambapo Yanga ilitinga hatua ya fainali ambayo ilishindwa kutwaa ubingwa licha ya kutoka sare ya mabao 2-2 na USM Alger ya Algeria.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live