Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kocha aliepewa "Thank you" Ihefu anukia Singida Big Stars

Katwila WA0011 Zuberi Katwila

Sat, 14 Oct 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Wakati klabu ya Ihefu na Kocha Zuberi Katwila wakithibitisha kufikia tamati kwa mkataba baina yao kwa makubaliano binafsi, habari za uhakika ambazo Mwanaspoti limezinasa ni kuwa kocha huyo anaenda kujiunga na Singida Big Stars kama kocha msaidizi.

Kocha huyo anakaribia kujiunga na Singida ili kusuka benchi jipya la ufundi litakaloongozwa na kocha wa kigeni ambaye atatangazwa hivi karibuni, huku timu hiyo ikiwa katika mpango wa kuachana na Mathias Lule na Thabo Senong waliokuwa wanaiongoza baada ya kuondoka kwa kocha mkuu Ernst Middendorp.

"Kuna kocha kutoka Brazil anakuja kuchukua nafasi ya kocha mkuu na msaidizi wake atakuwa ni Zuberi Katwila. Mpango wa kumchukua Katwila ulianza muda mrefu, ndio maana tulianza kumchukua kocha wa makipa, Peter Manyika," kimefichua chanzo ndani ya Singida.

Jana Ijumaa Ihefu ilitangaza kuachana na Katwila aliyekuwa akiinoa kwa miaka mitatu tangu Oktoba 2020 alipojiunga akitokea Mtibwa Sugar, klabu aliyowahi kuichezea enzi zake akisukuma boli uwanjani.

"Uongozi wa timu yetu umefikia makubaliano ya pande mbili ya kuvunja Mkataba na aliyekua Kocha wetu Mkuu Zuber Katwila. Hata hivyo uongozi wa timu unamshukuru Kocha Katwila kwa wakati wote aliokua nasi ndani ya timu kama Kocha Mkuu tangu alipojiunga nasi mwaka 2020," ilisomeka taarifa ya klabu ya Ihefu iliyoongeza;

"Ihefu Sc inamtakia kila la kheri Kocha Katwila katika maisha yake mapya ya soka na atabaki kuwa Mwanafamilia wa MbogoMaji."

Kocha huyo aliliambia Mwanaspoti kuwa kwa sasa yuko huru kujiunga na timu yoyote na kuhusu Singida Big Stars bado hajafanya mazungumzo nao.

"Sijafanya mazungumzo na timu yoyote ila itakayokuwa tayari kunihitaji tukakubaliana mimi niko tayari hata Ihefu naweza kurudi kwa sababu sijaondoka kwa ubaya zaidi ya makubaliano," amesema Katwila, huku Ofisa Habari wa Singida, Hussein Masanza amekiri pamoja na mkakati wao wa kuboresha benchi la ufundi lakini suala la Katwila wanaliona mitandaoni.

"Taarifa za Kocha Katwila tumeziona mtandaoni lakini sisi hatujamtangaza, tupo kwenye mazungumzo ya mwisho na kocha tutakayemleta tena kutoka nje hivyo tusubiri muda utaamua na uongozi tutatangaza," amesema Masanza.

Hadi anaondoka Ihefu, kwa msimu huu kocha huyo ameiongoza timu hiyo katika mechi tano na kushinda mbili, ikiwamo ile waliyoitibulia Yanga kwa kuwafunga mabao 2-1, ikiwa ni msimu wa pili mfululizo kwenye Uwanja wa Highland Estate, Mbarali kwani hata msimu uliopita ilifanya kama hivyo. Pia timu hiyo imepoteza mechi tatu ukiwamo wa mwisho wa ugenini dhidi ya KMC.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live