BAADA ya kuibuka na ushindi wa bao 1-0 nyumbani dhidi ya Polisi Tanzania juzi, Kocha mkuu wa timu ya Mbeya City, Mathias Lule amesema Namungo wasitarajie mteremko katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara, unaopigwa katika Uwanja wa Majaliwa, Ilulu mkoani Lindi leo.
Mbeya City wanaoshika nafasi ya 17 katika msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara wamejikusanyia pointi 24 watakuwa na kibarua kizito mbele ya Namungo wanaoshika nafasi ya 11 katika msimamo wakiwa na pointi 31 baada ya kucheza mechi 21.
Akizungumza na gazeti hili jana, Lule alisema kuwa ushindi alioupata katika mchezo uliopita dhidi ya Polisi Tanzania, umewarudishia hali ya kujiamini kikosini hivyo licha ya kuwa watakuwa ugenini wenyeji wao wasitarajie kupata pointi kirahisi kwani kikosi chake kimesheheni wachezaji wazuri.
“Najua utakuwa mchezo mgumu wenye presha kubwa kwetu tuko ugenini wapinzani wetu watakuwa wakisaka ushindi kwa nguvu lakini naamini tunaenda kufanya vizuri na kurejea na pointi tatu nyumbani,” alisema Lule.
Alisema kuwa malengo yao ni kubaki Ligi Kuu hivyo wanapaswa kupambana kwa nguvu kuhakikisha wanaondoka na pointi tatu katika mchezo huo ili kuendelea kusogea juu ya msimamo na kujiondoa katika ukanda wa kushuka daraja.