Kutokana na kichapo alichokipata kutoka kwa Simba Sc cha goli 2-0 usiku wa jana Kocha Mkuu wa Tabora United, Masoud Djuma amesema kwake haikuwa rahisi kucheza na Yanga na Simba timu ambazo moja inataka ubingwa moja inataka nafasi ya pili
Masoud Djuma, licha ya timu yake kuwa kwenye hali mbaya katika msimamo wa ligi, lakini anaamini kuna kitu anaweza kukifanya na timu yake isishuke daraja.
“Ukishafungwa mechi kama hii hakuna kitu kingine utasubiri kukipigia mahesabu zaidi ya mechi inayofuata, tunakwenda kucheza na Mtibwa kwao, mechi ngumu zaidi ya hizi zote. Mtibwa ni timu ambayo iko nyuma yetu kwenye msimamo, ni ngumu sana lakini tutazidi kupambana.
“Tumetoka kucheza na Yanga, sasa tumecheza na Simba, haikuwa rahisi kucheza na timu mbili, moja inataka ubingwa na nyingine inataka nafasi ya pili ukitazama na ubora wa timu hizo. Kikubwa tumemaliza mechi salama, tunakwenda kujipanga na mchezo ujao dhidi ya Mtibwa tuone kama tutapata ushindi.
“Hatuwezi kubaki tunalalamika., lazima tukubali matokeo na tukafanye kwa vitendo, hatuna jingine zaidi ya kusaka ushindi dhidi ya Mtibwa ili tujiweke kwenye nafasi nzuri. Tunakwenda kupambana,” amesema Kocha Masoud.