Kocha wa klabu ya Mamelodi Sundowns, Rulani Mokwena amesema kwa kujiamini kuwa watafuzu katika hatua ya Nusu Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika mbele ya Young Africans SC.
Young Africans na Mamelodi Sundowns zimetoka sare ya bila kufungana (0-0) katika mchezo wa kwanza wa Robo Fainali uliopigwa kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
"Bila shaka mtaiona Sundowns katika raundi inayofuata, nina uhakika sana kuhusu hilo, kwa kweli. Mpango ni kufika nyumbani salama, kupumzika na kuchambua mchezo huu na kisha kujiandaa" alisema Mokwena
Mchezo wa marudiano kati ya Sundowns dhidi ya Young Africans utapigwa Aprili 5, 2024 katika dimba la Loftus Versfeld katika kitongoji cha Arcadia, Pretoria katika mkoa wa Gauteng nchini Afrika Kusini.