Kocha Msaidizi wa Kagera Sugar, Marwa Chamberi amesema kuwa mchezo wa kesho wa ligi dhidi ya mabingwa watetezi, Yanga utakuwa mgumu kutokana na kwamba waliwazuia kupata ushindi katika duru ya kwanza kule Kaitaba Stadium.
Chamberi amesema hayo leo wakati akizungumza na wanahabari kuelekea mchezo huo utakaopigwa kesho katika Dimba la Azam Complex, Chamazi.
“Yanga wana kikosi kikubwa huwezi kujua nani ataanza na hata wanaoingia kama sub nao wana kiwango kama kilekile, wana kasi kwenye eneo lao la kushambulia wakiwa kwenye nusu yako lazima uwe makini.
“Yanga wanafanya rotation kubwa kwa hiyo wapo fiti na hujui nani atakufunga, kiufupi wanatuchanganya, kwa hiyo usipokuwa makini utapata shida.
“Sisi tutawakosa wachezaji wetu wawili, Cleophace Mkandala na Datius Peter wana majeraha.
“Kiuhalisia lazima kwanza tuwaheshimu Yanga, tutacheza kwa transition, wakipoteza mpira tutashambulia kwa kushitukiza,” amesema Chamberi.