Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kocha: Huyu Saido habahatishi

Saidoo Saido Ntibazonkiza

Thu, 3 Mar 2022 Chanzo: www.mwanaspoti.co.tz

Saido Ntibazonkiza amewasha huko Yanga na benchi la ufundi limewaambia mashabiki hicho anachokifanya habatishi wala si moto wa kifuu.

Kwa mujibu wa Kocha Msaidizi wa Yanga, Cedrick Kaze kiwango cha Saido kimepanda kutokana na kuwa na fiziki nzuri kwa sasa ambayo imemwongezea morali na amepania kufanya jambo la tofauti.

Kocha huyo aliyekaa Barcelona kwa miaka kadhaa, ameliambia Mwanaspoti mchezaji huyo ni mzoefu wa ligi za Afrika hivyo akiwa fiti kifiziki amekuwa akifanya mambo ya tofauti sana uwanjani akishirikiana na wenzie wanaomwelewa vilivyo kuanzia mazoezini.

“Saido akiwa vizuri kwenye fiziki ni mchezaji mzuri sana, ana akili ya mpira na anajua kuamua mechi,” alisema Kaze ambaye ndiye aliyemsajili kikosini hapo.

Kocha huyo alisema kila mchezaji ndani ya timu hiyo kwa sasa ana morali kubwa ya kupigania mafanikio na kulinda hadhi ya timu, ndio maana wamekuwa wakizidi kupepea kila mara na wanatambua umuhimu wa hatua waliyopo katika mbio za ubingwa.

“Bado tuna mwendo mrefu lakini angalau njia inaonekana kufikia mafanikio,” aliongeza Kaze ambaye ni muumini wa soka la pasi.

KIWANGO CHAKE

Katika mabao sita aliyoyafunga kati ya 23 iliyonayo Yanga katupia kwa aina tatu, faulo, penalti na muvu. Mabao sita ya Saido yamefungwa katika viwanja vitano, nje na kufunga pia ametoa asisti tano.

Alifunga dhidi ya Namungo FC bao la penalti dakika ya 80 iliyotokana na beki Emmanuel Charles kumchezea rafu Feisali Salum ‘Fei Toto’ dakika ya 79, mchezo ukimalizika kwa 1-1, Uwanja wa Majaliwa, ilikuwa Novemba 20.

Bao la faulo alilopiga nje kidogo ya 18 dhidi ya Mbeya Kwanza dakika ya 17, alianza kuucheza mpira mwenyewe, kisha akampa pasi Fei Toto aliyechezewa rafu na mabeki na dakika 90 ziliamua Yanga kushinda 2-0, ilikuwa Novemba 30, Uwanja wa Sokoine.

Penalti nyingine, Saido alifunga dhidi ya Biashara United dakika ya 79 Uwanja wa Benjamin Mkapa, ilitokana Jesus Moloko kuchezewa rafu na Abdulmajid Mangaro, Yanga ikishinda 2-1, Uwanja Benjamin Mkapa, Desemba 26.

Alifunga bao kali la muvu katikati ya mabeki wa Coastal Union dakika ya 89, baada ya kupokea pasi ya Faridi Mussa, Uwanja wa Mkwakwani, Yanga ikishinda 2-0 Januari Mosi. Bao lingine la aina hiyo ni dhidi ya Mtibwa Sugar dakika 45+5, Februari 23, Uwanja Manungu, timu yake ikishinda 2-0.

Bao la tatu la muvu ni dhidi ya Kagera Sugar dakika ya 64 na alipita katikati ya mabeki wawili akiukokota mpira, huku akimhadaa kipa kutoka golini kisha akapiga shuti kabla ya kufika ndani ya 18, Yanga ikishinda 3-0, Uwanja wa Benjamin Mkapa, Februari 27.

Tofauti na aina tatu za ufungaji wa Saido ambaye amekuwa akisisitiza ameiacha miguu yake izungumze, katika mabao yake sita, mawili ni ya penalti, moja faulo na matatu muvi.

Yanga imepania kubeba ubingwa msimu huu ambao imesajili mastaa ghali na wenye uzoefu kutoka kwenye nchi mbalimbali za Afrika.

Chanzo: www.mwanaspoti.co.tz