Kocha Mkuu wa Al Ahly, Marcel Koller, amesema yaliyotokea huko nyuma yamepita na sasa wanachoangalia ni kushinda mchezo wao wa kesho dhidi ya Simba SC.
Kocha huyo ametoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza na wanahabari hii leo Oktoba 19, 2023 kuhusu mchezo huo wa kwanza wa robo fainali ya Ligi ya African Football.
"Tunafurahi kuwa hapa (Tanzania) kucheza mechi ya ufunguzi wa mashindano ya African Football League, nafahamu historia ya Al Ahly ikicheza hapa, tunajua mechi itakuwa ngumu kwa sababu tunakutana na timu ngumu hususan kila timu Afrika inapokutana na Al Ahly wachezaji wake wanahamasika mara mbili zaidi.
Nipo Al Ahly kwa mwaka mmoja sasa, yaliyotokea huko nyuma tayari yamepita na huwezi kubadilisha, yaliyopita yamepita tunachoangalia ni leo na kesho. Tumejiandaa kuhakikisha tunafanya kila tunaloweza kesho kupata ushindi na kubadilisha historia," alisema Marcel.