LICHA ya kuwa Yanga wana nafasi ya kufanya vizuri kwenye mchezo wa marudiano na kuingia makundi hapo kesho Jumamosi dhidi ya Zesco United kwenye Ligi ya Mabingwa kuna timu ambazo nafasi zake ni finyu.
Yanga wanatakiwa kuibuka na ushindi wa aina yoyote uwanja wa Levy Mwanawasa, Ndola nchini Zambia ambako utachezwa mchezo wa marudiano ili kusonga mbele hatua ya makundi, ambayo msimu uliopita Simba walitinga.
Katika mchezo wa awali baina ya Yanga na Zesco United, inayonolewa na George Lwandamina ulimalizika kwa sare ya bao 1-1, uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaaam.
Gor Mahia ya Kenya na Côte d'Or FC ya Shelisheli ni miongoni mwa timu ambazo kidizaini ni kama zimegeukia mlango wa kutokea kwenye michuano hiyo kutokana na matokeo ya michezo yao ya kwanza.
Licha ya kuwa Gor Mahia walikuwa ugenini, kipigo cha mabao 4-1 kutoka USM Alger ya Algeria kimewaweka njia ya panda kwa sababu wanatakiwa kushinda mabao 3-0 ili waingie makundi kitu ambacho si rahisi mbele ya Waarabu hao.
Maajabu ambayo yanatakiwa kufanywa na Côte d'Or FC ya Shelisheli hayawezi kukuingia hata kidogo akilini, maana walitandikwa kwao na Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini mabao 5-0 ina maana wanatakiwa kupindua matokeo ugenini.
Lolote linaweza kutokea kwenye michezo mingine ambayo inachezwa leo, kesho huku wale ambao watatolewa kwenye raundi hii ya kwanza watahamia Kombe la Shirikisho Afrika
Mechi zitakazopigwa leo Ijumaa ni kati ya Espérance de Tunis watakuwa kwao Tunisia kucheza na Elect-Sport saa 3:00 usiku, KCCA ya Uganda itacheza na Petro de Luanda ya Angola saa 10:00 jioni huku Mamelodi Sundowns wakicheza na Côte d'Or saa 2:00 usiku.