Baada ya ushindi wa bao 1-0 wa Mamelodi Sunsowns dhidi ya Pyramids FC iliyokuwa nyumbani kwenye Uwanja wa June 30, Cairo, Misri, mchezo wa nne wa kundi A, Ligi ya Mabingwa Afrika, kiungo wa timu hiyo, Teboho Mokoena amemjibu Fiston Mayele kwa kile alichoandika kwenye akaunti yake ya Instagram.
Mayele baada ya kushindwa kusafiri na timu yake ya Pyramids FC kwenda Afrika Kusini kwenye mchezo wa kwanza, aliandika; "Sawa ulikataa kunipa visa ukiamini utatupiga subutu, pointi 1 muhimu tukutane sasa Cairo."
Sasa baada ya matokeo ya ushindi wa Mamelodi, Mokoena amejibu kwenye posti hiyo iliyoandikwa wiki moja zilizopita,
“Ulikuwa unasema?”, ikiwa ni kijembe kwa nyota huyo aliyewahi kutamba na Yanga akiifikisha fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika.
Katika kundi hilo, Memolodi inaongoza na pointi saba sawa na TP Mazembe huku Pyramids ikiwa nafasi ya tatu na pointi nne sawa na Nouadhibou.