Aliyekuwa Kocha Mkuu wa Namungo, Denis Kitambi amekuwa lulu sokoni baada ya klabu za Geita Gold na Ihefu kumhitaji.
Kitambi aliyeachana na Namungo Desemba 13, mwaka huu alikuwa ni kocha wa pili kuondoka katika timu hiyo baada ya awali Mrundi, Cedric Kaze kuondoka pia Oktoba 22 mwaka huu kutokana na kikosi hicho kuandamwa na matokeo mabaya ya Ligi Kuu.
Ofisa Habari wa Geita Gold, Samwel Dida alisema ni kweli Kitambi ni miongoni mwa makocha wanaozungumza nao ingawaje mezani kwao wako watatu hadi sasa na wanaendelea kuwachuja mmoja baada ya mwingine.
“Programu za timu zinaendelea na Kocha Hemed Suleiman ‘Morocco’ ila kutokana na majukumu yake kwenye timu yetu ya taifa tunaweza tukaboresha eneo hilo na waliojitokeza mbali na Kitambi ni Fredy Felix ‘Minziro’ na Francis Baraza,” alisema.
Kwa upande wa Ofisa Habari wa Ihefu, Peter Andrew alisema baada ya kuondoka, Moses Basena hawana haraka na mchakato wa kumpata kocha mpya kwa sasa na suala la kumuhitaji Kitambi kwao halipo kwa sababu hawajawahi kufanya mawasiliano naye.