Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kisa kwenda Yanga, Simba na Chama wapelekana TFF

Chama Yanga 003 Clatous Chama.

Tue, 16 Jul 2024 Chanzo: Mwanaspoti

Kama ulidhani ishu ya Clatous Chama kutambulishwa ndani ya kikosi cha Yanga kisha kuanza mazoezi tangu wiki iliyopta ni rasmi amekuwa mchezaji wa timu hiyo, taarifa mpya ni kwamba nyota huyo bado hajamalizana na Simba ambao wameonekana kuweka ngumu kiasi cha ishu yao kutinga katika ofisi za Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).

Taarifa ilizozipata Mwanaspoti zinabainisha kwamba, mpaka sasa Simba haijampa Chama barua ya kumuachia licha ya kwamba nyota huyo amemaliza mkataba wake ndani ya kikosi hicho.

Chama ambaye alianza kuitumikia Simba mwaka 2018 akitokea Lusaka Dynamos ya kwao Zambia, ameondoka Simba mwishoni mwa msimu uliopita baada ya mkataba wake kumalizika na kutambulishwa Yanga Julai Mosi, mwaka huu.

Mwanaspoti linafahamu kwamba, leo Jumanne, Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji inakutana pale kwenye ofisi za TFF zilizopo Ilala jijini Dar es Salaam kupitia mashauri kadhaa yaliyopo mezani kwao.

Mtoa taarifa wetu amebainisha kwamba, miongoni mwa mambo ambayo leo yatajadiliwa, ni ishu ya Simba mpaka sasa kushindwa kutoa barua ya kumuachia Chama ili aidhinishwe rasmi ndani ya Yanga huku taarifa zikibainisha kwamba upande wa mchezaji ndiyo umewasilisha malalamiko hayo.

"Simba mpaka sasa hawajampa Chama barua ya kumuacha awe huru baada ya kumaliza mkataba nao, hili suala limefikishwa kwenye kamati na ni miongoni mwa yatakayojadiliwa katika kikao cha kesho (leo) pale TFF," kilisema chanzo hicho.

Mwanaspoti lilifanya juhudi za kuwasaka viongozi wa Simba na Yanga kuzungumzia ishu hiyo, lakini hawakuwa tayari kuweka wazi huku wakisubiri uamuzi wa kamati.

Chanzo: Mwanaspoti