KIPA wa Biashara James Ssetuba baada ya kumalizika kwa mechi ya Ligi Kuu Bara kati ya timu yake na Simba (0-0), amejikuta akipewa pesa na mashabiki kwa kiwango bora alichokionesha.
Ssetuba aliibuka nyota wa mchezo huo baada ya kupangua penalti ya dakika ya mwisho ya mchezo huo iliyopigwa na John Bocco na kufanya mechi hiyo kumalizika kwa suluhu ya bila kufungana.
Baada ya mchezo kumalizika, Ssetuba alijikuta akioga noti kutoka kwa mashabiki wa timu hiyo waliokuwa wamekaa VIP wakimshangilia na kumpa pesa kila mmoja kwa uwezo wake.
Akizungumza na Mwanaspoti baada ya kuidhibiti Simba kupata bao hata moja leo, Ssetuba amesema huo ni mwanzo tu na mambo mazuri yanakuja.
“Nashukuru kwa kuwa na mchezo mzuri leo, pia nawapongeza wachezaji wenzangu kwa upambanaji waliouonesha hadi tumepata alama moja. Nadhano huu ni mwanzo tu na mambo mazuri yanakuja,” amesema Ssetuba.
Baada ya hapo kipa huyo raia wa Uganda aliondoka na meneja wa timu hiyo na kwenda katika vyumba vya kubadilishia nguo kuungana na wenzake.