Wakala mkubwa wa soka duniani, Mino Raiola (54) amefariki dunia baada ya kuugua kwa muda mrefu jijini Milan alikokuwa amelazwa tangu Januari, mwaka huu.
Familia ya wakala huyo anayesimamia nyota wengi maarufu wa soka kama vile Paul Pogba, Marco Verratti, Erling Haaland, Zlatan Ibrahimovic, Gianluigi Donnarumma na Matthijs de Ligt ilitoa taarifa jana ya kifo chake ambaye imepokelewa kwa huzuni kubwa na wadau wa soka duniani.
“Kwa masikitiko makubwa tunawajulisha kuondokewa na aliyekuwa wakala wa kipekee na anayejali kupitiliza. Mino amepigana hadi mwisho kwa uimara uleule aliouweka katika meza ya makubaliano kuwalinda wachezaji wetu.”
“Tunamshukuru kila mmoja kwa sapoti kubwa tuliyopokea katika nyakati hizi ngumu na tunaomba heshima ya usiri kwa familia na marafiki katika nyakati hizi za huzuni,” ilifafanua familia ya wakala huyo.
Kifo cha Raiola kimetokea siku chache tangu kulipoibuka tetesi za wakala huyo kufariki dunia ambazo hata hivyo zilikanushwa kwa nguvu na familia yake.
Taarifa za kifo cha wakala huyo zimepokelewa kwa majonzi makubwa na klabu za soka, wachezaji, wachambuzi, waandishi wa habari za michezo pamoja na mashabiki wa soka ambao wametuma salamu nyingi za rambirambi na jumbe za kuonyeshwa kuguswa na kifo chake.
Baadhi ya waliotuma salamu hizo ni klabu za PSG, Inter Milan, Real Madrid na Nice huku watu maarufu baadhi wakiwa ni Fabrizio Romano na David Ornstein