Straika wa Man City, Erling Haaland hakufua dafu kabisa mbele ya mabeki wa Arsenal kwenye mchezo wa Ligi Kuu England na jambo hilo limemfanya akosolewe vikali na gwiji wa ligi hiyo na nahodha wa zamani wa Manchester United, Roy Keane.
Keane alimchambua vibaya straika Haaland na kulinganisha kiwango chake na wachezaji wa League Two baada ya kushindwa kufanya kitu cha maana uwanjani katika mechi ambayo alipaswa kufanya kweli na kuisaidia timu yake kwenye mbio za ubingwa, alisema:
“Kiwango chake cha uchezaji ni duni sana. Na sio kwenye mechi hii tu. Akiwa mbele ya goli, Haaland ni bora duniani, lakini kwa upande wa uchezaji kama mchezaji ni hovyo sana. Anapaswa kubadilika. Anakaribia kuwa na kiwango cha mchezaji wa League Two (Ligi Daraja la Pili) hivyo ndivyo ninavyomwona. Uchezaji wake kwa ujumla anapaswa kubadilika. Ni straika mzuri lakini abadilike uchezaji wake. Ni hivyo.”