Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kaze awashusha presha Yanga

9163516c7e19287187eb988af6555bb1.jpeg Kaze awashusha presha Yanga

Tue, 24 Nov 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

KOCHA wa Yanga, Cedric Kaze amewashusha presha mashabiki wa timu hiyo akisema kikosi chake kipo tayari kwa mchezo dhidi ya Azam FC unaotarajiwa kufanyika kesho kwenye Uwanja wa Azam Complex Dar es Salaam.

Kaze alitoa kauli hiyo juzi baada ya timu yake kulazimishwa sare ya bao 1-1 na Namungu katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliofanyika kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa.

Sare ya juzi ni ya tatu mfululizo kwa Yanga baada ya kutoka suluhu na Gwambina na sare ya 1-1 na Simba.

“Najua mchezo utakuwa mgumu kwakuwa tunaenda kucheza na timu inayoongoza ligi na sisi tutaingia kwa lengo la kutafuta ushindi kutafuta pointi zitakazotuweka mbele,” alisema Kaze.

Azam ina pointi 25 sawa na Yanga lakini inaongoza msimamo kwa uwiano mzuri wa mabao.

Alisema ugumu wa mchezo huo unatokana na Azam kupoteza mechi iliyopita na timu yake kupata sare hivyo kila mmoja ataingia uwanjani kutaka ushindi licha ya kuwa na muda mchache wa maandalizi.

Kaze alisema mchezo uliopita dhidi ya Namungo wachezaji wake hawakuwa kwenye kiwango bora kwani walikuwa wanawaacha huru wapinzani wao na walikuwa wanatengeneza mipango iliyowapa bao la kusawazisha.

Alisema hata kwenye mchezo unaokuja kikosi chake kitakuwa kinabadilika kwakuwa kuna baadhi ya wachezaji anawapatia majukumu ya namna ya kucheza lakini wanaonekana kushindwa kwakuwa hivyo anakikosi kipana atakuwa anawapa nafasi wengine kujaribu.

Katika mchezo dhidi ya Namungo bao la Yanga lilifungwa dakika ya 13 na Carlos Fernandes’Carlinhos’, wakati wapinzani wao walisawazisha dakika ya 16 kupitia Stephen Sey baada ya kuwadanganya walinzi na kuachia shuti kali lilomuacha kipa Metacha Mnata akiwa hana la kufanya.

Naye kocha wa Namungo FC, Hemed Morocco alisema kikosi chake kinasumbuliwa na wachezaji wa kutofunga akitolea mfano kwenye mchezo huo walitengeneza nafasi 11 za wazi lakini walitumia moja.

“Ilikuwa mechi ngumu lakini nawashukuru vijana kwa kucheza kwa kufuata maelekezo niliyowapa ingawa tulistahili kupata ushindi,” alisema Morocco.

Alisema makosa yaliyojitokeza kwenye mchezo huo atayafanyia kazi kujipanga na michuano ya kimataifa ya Kombe la Shirikisho Afrika.

Chanzo: habarileo.co.tz