KOCHA wa Yanga, Cedric Kaze amewapongeza wachezaji wake kwa kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Azam FC katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliochezwa kwenye Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam juzi.
Matokeo hayo yanaifanya Yanga kuongoza ligi kwa pointi 28 na kuishusha Azam nafasi ya pili iliyobaki na alama zao 25, huku timu zote mbili zikiwa zimecheza michezo 12.
Akizungumza baada ya kumalizika mchezo huo, Kaze alisema matokeo ya mchezo huo yamewapa nguvu kwani wametimiza azma yao ya kuongoza ligi baada ya kupambana kwa muda mrefu.
“Mchezo ulikuwa muhimu kushinda, tumepata pointi tatu tunashukuru Mungu na tulistahili kwa namna ambayo tulipambana, tulikuwa bora kwenye safu ya ulinzi na kuzuia wapinzani wetu wasipige mashuti kwenye eneo letu.”
“Nawapongeza wachezaji kila mmoja alicheza na kutimiza wajibu wake kupigana kuhakikisha timu inapata ushindi,” alisema.
Hata hivyo, Kaze alisema kikosi chake kinahitaji kuongezewa kujiamini ili kipate morali na kufunga mabao mengi kwenye michezo inayokuja na waache kuridhika na ushindi wa bao moja kila mchezo.
“Kocha yeyote duniani hafurahii kuona hivi, unaweza kuumwa hata miaka 40, napambana kuona hali hii inakwisha ili kwenye michezo inayokuja tupate mabao mengi,” alisema Kaze.
Naye Deus Kaseke ambaye alifunga bao pekee kwenye mchezo huo ametamba kuwa kufanya mazoezi na kuzingatia maelekezo ya kocha ndio sababu ya kucheza vizuri kwenye mchezo huo.
“Napambana kufanya mazoezi kwa kujituma na kufuata maelekezo tunayopewa na kocha ndio sababu iliyonifanya kucheza vizuri kwenye mchezo huu ambao ulikuwa na presha kubwa,” alisema.