By Olipa AssaMore by this Author MBINU mpya za Kocha wa Yanga, Cedrick Kaze kumpa nafasi kila mchezaji ndani ya kikosi chake cha kwanza, wadau wa soka wamekitafsiri kama silaha kali ya kuleta ushindani kwa mastaa wake kuwa fiti na kuisaidia timu kupambania ubingwa.
Straika wa zamani wa Yanga na Simba, Edbily Lunyamila alisema Deus Kaseke lazima atazamwe kwa jicho la tatu ndani ya kikosi cha Yanga, kutokana utendaji wake kuibeba timu katika mazingira magumu na pia anatimiza majukumu kama anavyopangiwa na kocha.
Alisema anaamini mfumo wa kocha Cedrick Kaze wa kuandaa kikosi cha kucheza mazoezini, kutaisaidia Yanga kuwa na mastaa wanaoshindana na nidhamu ya kazi, itakayowapa nguvu ya kutwaa ubingwa kwa msimu huu.
“Kikosi cha Kaze hakipangwi kimazoea, kuona mchezaji anakubalika na mashabiki, anawashindanisha mazoezini, hilo ni jambo litakalompa mafanikio ya kuwa na wachezaji wenye mazoezi ya kutosha na nidhamu ya kuheshimu kazi,” alisema na aliongeza kuwa;
“Kaseke asingekuwa anaonyesha kujituma mazoezini sijui kama angekuwa anapewa nafasi katika kikosi cha kwanza, namuona anafanya vizuri sana na ndio maana anaongoza kwa mabao matano kwenye kikosi cha Yanga,” alisema.
Oscar Joshua beki wa zamani wa timu hiyo, aliunga mkono hoja ya Lunyamila kwamba Kaseke anastahili kupewa heshima yake kwa namna anavyoonyesha moyo wa kizalendo wa kuipambania Yanga kuipa matokeo kwenye nyakati ngumu.