Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kasi ya Yanga yawalaza macho Vigogo Simba SC

Try Again, Salim Abdallah Mwenyekiti wa Bodi, Salim Abdallah ‘Try Again’.

Mon, 21 Mar 2022 Chanzo: www.mwanaspoti.co.tz

Kas ya Yanga kwenye Ligi Kuu Bara imeshtua mabosi wa Simba na juzi waliamua kuitana na kujifungia kwa muda wa saa kama mbili jijini Dar es Salam ili kuijadili, sambamba na kuweka mikakati ya kuhakikisha hawakubali kupoteza mataji yao ya Ligi Kuu Bara na Kombe la Shirikisho (ASFC).

Simba ndio watetezi wa Ligi Kuu ikishikilia taji kwa misimu minne mfululizo na Kombe la ASFC kwa misimu misimu miwili mfululizo, lakini Yanga ya msimu huu imeonekana kuwa moto ikitisha katika Ligi Kuu ikiwa kinara, huku ni miongoni mwa timu zilizinga robo fainali ya Kombe la ASFC.

Katika kuhakikisha mambo hayawaharibikii, vigogo wa klabu ya Simba walikutana juzi jijini Dar es Salaam kuijadili Yanga, licha ya kuwepo na ajenda nyingine muhimu ya kuhakikisha inafanya vizuri kwenye michuano ya CAF wakilenga kutaka kuona timu hiyo inafika nusu fainali na hata kubeba ubingwa kabisa.

Licha ya vikao hivyo vya Bodi ya Wakurugenzi ya klabu hiyo kufanyika mara kwa mara lakini cha juzi kilichofanyika Dar es Salaam kilikuwa na ajenda saba huku ya kutetea mataji mawili na michuano ya kimataifa zikichukua muda mrefu kujadiliwa kutokana na kasi ya Yanga kuwashtua msimu huu.

Mwanaspoti lilipenyezewa kuwa, katika kikao hicho kilichoongozwa na Mwenyekiti wa Bodi, Salim Abdallah ‘Try Again’ kiliudhuliwa na wajumbe wote wa bodi na kujadili mambo mengi yanayohusu timu yao.

Chanzo chetu cha habari kilisema, kutwaa taji la ligi mara ya tano mfululizo ambalo Yanga inahaha kwa udi na uvumba kulichukua kulizungumziwa na namna gani ya kutimiza lengo hilo.

“Tulikuwa na ajenda saba kufungua kikao, Ubingwa wa ligi kuu, FA, michuano ya kimataifa, ubingwa Simba Queens, Mengineyo na kufunga kikao, tulijadili juu ya kombe la ASFC, sisi kama watetezi tunataka kulibeba tena kwa msimu wa tatu mfululizo,” alisema mtoa habari huyo.

Jambo lingine ambalo bodi ilijadili na kulipitisha ni ushiriki wa Simba katika michuano ya Kimataifa ambapo malengo ya sasa ni kufika nusu fainali baada ya kudondoshwa katika Ligi ya Mabingwa.

“Uwezo tunao kabisa wa kufanya hivyo, na ndio maana malengo ya awali ilikuwa kutinga makundi tumefanikiwa, tunaenda robo fainali na tunaamini tutafika nusu fainali kwa uwezo wetu na Mungu pia,” alisema.

Mwanaspoti lilimtafuta Mjumbe wa Bodi hiyo, Asha Baraka ‘Iron Lady’ juu ya kikao hicho naye alikiri ni kawaida yao kufanya vikao lakini kilichojadiliwa kinabakia kuwa siri yao kwa manufaa ya klabu yao.

“Umepata wapi hizo habari za kikao chetu cha ndani, ni kawaida tu kukutana lakini tunayoyajadili yanabakia kwetu kwa sababu ni mipango yetu,” alisema Asha ambaye alizungumzia mchezo wa leo wa timu hiyo dhidi ya Asec Mimosas ya Ivory Coast kwamba licha ya kuheshimu wako ugenini na watapambana kufanya vizuri.

“Tayari Mwenyekiti wetu wa bodi ametimkia Benin na wajumbe wengine lengo kuu ni kuhakikisha tunapata matokeo kuweza kufikia malengo yetu,” alisema Asha.

Chanzo: www.mwanaspoti.co.tz