Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kamati ya Taifa Stars yazua mjadala mzito

Mwijaku Na Baba Levo Wazichapa Mbele Ya Waandishi.png Mwijaku na Baba Levo.

Fri, 5 Jan 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Wadau wa soka nchini wamekuwa na mitazamo tofauti kuhusu Kamati Maalumu kwa ajili ya hamasa kwa timu za taifa iliyoundwa juzi na Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Damas Ndumbaro kwa lengo la kuhamasisha katika mashindano mbalimbali.

Katika kamati hiyo iliyotangazwa juzi inaundwa na Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti, Katibu na Wajumbe 16 itakuwa na jukumu kubwa la kuhamasisha mashabiki na wapenzi wa michezo ndani na nje ya nchi kujitokeza kuzishangilia na kuziunga mkono timu za taifa.

Pia, itaratibu hafla maalumu ya harambee ya kuzichangia itakayofanyika Januari 10, mwaka huu jijini Dar es Salaam kwenye Hoteli ya Johari Rotana na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa atamwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan.

Hii si mara ya kwanza kwa serikali kuunda kamati za aina hiyo, kwani mwaka 2019 Stars iliposhiriki fainali za Afcon zilizofanyika Misri na kumaliza mkiani mwa kundi ililopangwa na Algeria, Senegal na Kenya iliundwa pia.

Kamati ya sasa inaundwa na Theobald Sabi (Mwenyekiti), Patrick Kahemela (Makamu Mwenyekiti) na Neema Msitha (Katibu), huku wajumbe ni Beatrice Singano, Michael Nchimbi, Jemedari Said, Nick Reynolds ‘Bongo Zozo’, Hamis Ali na Christina Mosha ‘Seven’.

Wengine ni Injinia Hersi Said, Salum Abdallah ‘Try Again’, Paulo Makanza, Mohamed Soloka, Hassan Mohamed Raza, Lucas Mhavile ‘Joti’, Oscar Oscar ‘Mzee wa Kaliua’, Prisca Kishamba, Burton Mwemba ‘Mwijaku’ na Clayton Revocatus Chipondo ‘Baba Levo’.

Uteuzi wa wajumbe wa kamati hiyo umewaibua nyota wa zamani wa soka waliosema imejaa wachekeshaji na sio watu wa mpira na haiwezi kuisaidia Stars kufanya maajabu Ivory Coast na Twiga Stars itakayoshiriki fainali za Wafcon zinazofanyika Morocco baadaye.

Akizungumzia wajumbe hao nyota wa zamani wa timu ya taifa, Taifa Stars, Sekilojo Chambua alisema kwa upande wake anaona kamati imejaa wachekeshaji zaidi kuliko watu wenye uelewa na mpira ingawa hatambui waziri alitumia kigezo gani kuwateua.

“Binafsi sina shaka kabisa na ‘Bongo Zozo’, kuwepo kwa sababu ni mtu anayejitoa sana ila nimeshtuka kutoona hata jina moja la mchezaji wa zamani kwani ukiangalia Jemedari Said amechaguliwa kama mchambuzi na sio vinginevyo,” alisema.

Chambua aliongeza alitamani kuona watu kama Sunday Manara, George Masatu na wakongwe wengine kuwepo ila kumuona mtu kama Mwijaku kwenye vitu siriasi kwake binafsi anaona ni upungufu mkubwa na kamati hiyo haina mantiki.

Kwa upande wa mchezaji na kocha wa zamani wa Stars, Abdallah ‘King’ Kibadeni alisema ameshangazwa pia na kamati hiyo huku akihoji kutoona baadhi ya majina makubwa ya mastaa kama Madaraka Suleiman ambao wamekuwa na mchango mkubwa nchini.

Zamoyoni Mogella ambaye pia ameitumikia timu ya taifa alisema ameshindwa kuelewa kabisa kamati hiyo kazi yake kubwa hasa ni nini maana haoni wachezaji wa zamani wanaoweza kuwajenga waliopo zaidi anaona wanaenda tu kwa ajili ya vichekesho.

Wachezaji wengine waliotajwa ni kina Sunday Manara na Mtemi Ramadhani ambao wana upeo mkubwa na mchezo wa soka. Tanzania iliyopangwa Kundi F la michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON) inayoanza rasmi Januari 13 na kuisha Februari 11, huko Ivory Coast itaanza kampeni Januari 17 kwa kucheza na Morocco kwenye Uwanja wa Laurent Pokou, San Pedro.

Baada ya hapo itashuka tena Januari 21 kucheza na Zambia kisha kuhitimisha ratiba ya makundi kwa kupambana dhidi ya DR Congo Januari 24, kwenye Uwanja wa Amadou Gon Coulibaly, Karhogo.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live